Benki ya Exim Tanzania (Exim Bank) imekabidhi madawati 100 yenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 20, kwa ajili ya kusaidia kuondoa adha ya upungufu wa mawadati katika Shule mbalimbali za Msingi mkoani Mwanza.
Akizungumza tarehe 23 Novemba 2021 kwenye zoezi fupi la kukabidhi madawati hayo kwa uongozi wa Serikali mkoani Mwanza, Mkuu wa Kitengo cha Masoko na Mawasiliano kutoka Benki ya Exim, Stanley Kafu amesema hatua hiyo itasaidia kuboresha mazingira kwa wanafunzi kupata elimu.
Aidha amebainisha kuwa Benki ya Exim inaadhimisha miaka 24 tangu kuanzishwa kwake mwaka 1997 ambapo katika kusherehekea maadhimisho hayo imeanzisha mpango wa kutoa madawati 1,000 kote nchini ikiwa ni sehemu ya kurejesha shukurani kwa jamii.
“Miezi miwili iliyopita tulisherehekea miaka 24 tangu benki yetu ianze kutoa huduma ambapo tuliamua kutoa madawati 1,000 ili kwa kushirikiana na Serikali tusaidie kupunguza changamoto za elimu nchini. Tunashukuru Waziri Mkuu wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa aliuzindua mwezi uliopita mkoani Lindi hivyo tuko hapa kukabidhi madawati haya 100 ikiwa ni sehemu ya kutekeleza mpango huo,” amesema Kafu.
Kafu ameongeza kuwa Benki ya Exim mbali na kutoa huduma bora za kifedha pia ina nafasi kubwa ya kuboresha sekta mbalimbali za maendeleo katika jamii ikiwemo elimu ambapo hatua hiyo imechochea kuanzishwa kitengo maalum cha Exim Inajali (Exim Cares) kwa lengo la kushirikiana na Serikali pamoja na wadau mbalimbali kuboresha sekta hizo.
Akipokea madawati hayo, Mkuu wa Mkoa Mwanza Mhandisi Robert Gabriel ameipongeza benki ya Exim kwa kutimiza miaka 24 tangu kuanzishwa kwake na kuamua kureshesha fadhira kwa jamii kupitia madawati hayo kwani yatasaidia kuondoa uhitaji uliopo na kuboresha mazingira ya wanafunzi kujifunza.
“Madawati haya yataleta mageuzi makubwa kwenye mkoa wetu kwani uhitaji ni mkubwa, tuna miradi mingi ya ujenzi wa vyumba vya madarasa inayoendelea baada ya kupokea fedha nyingi kutoka kwa Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan hivyo natoa shukurani za dhati kwenu na naomba taasisi nyingine ziige mfano huu” amesema Mhandisi Gabriel.
Akipokea madawai hayo kutoka kwa Mkuu wa Mkoa Mwanza, Mkuu wa Wilaya Misungwi Veronica Kessy amesema kwa kushirikiana na viongozi wenzake atahakikisha madawati hayo yanakabidhiwa katika Shule zenye uhaba na kutunzwa vyema kwa lengo la kuleta tija iliyokusudiwa hususani kukabiliana na uhaba uliopo uliotokana na mwitikio wa wazazi kupeleka watoto Shule kutokana na sera ya elimu bila ada.
Naye Afisa Elimu Mkoa Mwanza, Mwalimu Martine Nkwabi amesema kwa Shule za Msingi na Sekondari kuna uhaba wa takribani madawati laki moja na elfu 80 (180,000) na kuongeza kuwa madawati 100 yaliyotolewa na Benki ya Exim yatasaidia kukabiliana na uhaba huo huku yakiwasaidia wanafunzi 300 kuwa na mazingira bora ya kukaa wakiwa darasani.
NA MWANDISHI WETU