The House of Favourite Newspapers

Bosi wa WhatsApp mwenye somo tamu la utajiri!

0

Jan KoumBAADA ya makala ya wiki iliyopita tulipomalizia mbinu kumi za kuwa kama tajiri namba moja Afrika, Aliko Dangote, tumejifunza kuwa watu wengi wanatamani kuwa matajiri lakini hawana elimu ya kutosha juu ya ujasiriamali. Ni kweli kwamba kila mtu anataka kuwa TAJIRI lakini wengi wanaona kama ni ndoto ambayo haiwezi kuwa ya kweli.

Kupitia ukurasa huu, kila wiki tutakufundisha jinsi ya kutafuta fedha ili uwe tajiri. Cha kufanya usikose kusoma hapa kila wiki na kwamba usiniangushe msomaji wangu. Yale ninayokupa hapa,
tafadhali nakuomba uyaweke kwenye vitendo kwa kadiri uwezavyo. Baada ya kusema hayo, nikuhakikishie kuwa unapozungumzia mitandao ya kijamii inayotumiwa na watu wengi duniani kwa sasa ni vigumu kuacha kuutaja Mtandao wa Kijamii wa WhatsApp. Mtandao huu ulianzishwa na jamaa aitwaye Jan Koum.

Koum ni Myahudi aliyezaliwa nchini Ukraine mwaka 1976. Alipofikisha umri wa miaka 16, alikwenda nchini Marekani kumsaidia bibi yake kazi kwani hakupenda kuishi Ukraine ambapo alimsaidia
mama yake kuuza vinywaji kwenye grosari.

Kwa kuwa alipenda kompyuta, akaamua kwenda kusomea kompyuta katika Chuo cha San Jose State cha Marekani, akisomea mambo ya programu za kompyuta.
Baada ya Mtandao wa Kijamii wa Yahoo kugundua kwamba jamaa alikuwa noma kwenye mambo ya programu, wakaamua kumpigia simu na kumwambia aende kuanza kazi. Huko ndiko alipokutana na jamaa aitwaye Brian Acton.

AACHANA NA SHULE
Kipindi alichokuwa akifanya kazi, pia alikuwa akisoma chuo kama kawaida. Siku moja kuna ‘server’ ya Yahoo ilikorofisha, mkurugenzi wake, David Filo (mwanzilishi wa Yahoo) akampigia simu Koum na kumuuliza: “Upo wapi?” Jamaa akajibu kuwa alikuwa shuleni. Filo akamwambia aachane na shule hivyo aende ofisini kwake haraka iwezekanavyo. Wataalam wote waliokuwa ofisini, walishindwa kutengeneza hivyo alihitajika yeye, alipofika, akajitetea kwa bosi wake kwamba yeye mwenyewe alikuwa hapendi shule, hivyo akaachana nayo.

AONDOKA YAHOO
Baadaye jamaa alijiona anajua, mshahara aliolipwa haukuendana na kazi yake, hakutaka kuomba kuongezwa, hivyo mwaka 2007, aliamua kuacha kazi, hakuwa peke yake bali alikuwa na mshikaji wake, Acton.

TWITTER NA FACEBOOK ZAWATAKA, WACHOMOA
Baada ya kuacha kazi tu, Mitandao ya Kijamii ya Twitter na Facebook ikawataka kwenda kufanya nao kazi, jamaa wakakataa kwani hawakutaka kuwatajirisha watu wengine kupitia uwezo wao. Walichokifanya ni kujadiliana. Baada ya kukaa kwa muda, Koum akaamua kuanzisha WhatsApp huku akimfanya Acton kuwa meneja wa kampuni hiyo ndogo.

MARK ZUCKERBERG AANZA UKARIBU NAYE
Mtandao wa WhatsApp uliposhika kasi huku watu wengi wakijiunga nao, mwaka 2012 mwanzilishi wa Mtandao wa Facebook, Mark Zuckerberg akaamua kumtafuta Koum.

Alimpigia simu na kumtaka kuungana naye kwenye kula chakula cha usiku, alifanya hivyo, wakawa wanawasiliana kwa miaka miwili iliyofuata huku urafiki ukikua, kumbe mwenzake alikuwa akiutaka mtandao wake tu.

Mwaka 2014, Zuckerberg alimwambia Koum kwamba alitaka kuununua mtandao wake, jamaa akaomba muda wa kujifikiria. Ilipofika Februari 14, mwaka huo, jamaa hakutaka kuchelewa kwani fedha iliyowekwa mezani ilikuwa ndefu, akamfuata nyumbani kwake.

Wakazungumza na kukubaliana, mtandao uuzwe kwa Dola Bilioni 19 za Kimarekani (zaidi ya Sh. trilioni 35 za Kitanzania). Mtandao ukauzwa fastafasta huku siku iliyofuata jamaa kutoka Facebook akawafuata Koum na Acton, mtandao ukauzwa.

UTAJIRI WAKE SASA!
Leo unapomzungumzia Koum ambaye ni bosi wa WhatsApp, utakuwa unamzungumzia mtu mwenye utajiri wa Dola za Kimarekani Bilioni 8.9 (zaidi ya Sh. trilioni 18 za Kitanzania). Anashika nafasi ya 126 kwa utajiri duniani. Kama Koum ameweza, je, wewe unashindwa nini? Amka msomaji wangu, utajiri unalala nao!

Leave A Reply