The House of Favourite Newspapers

Chid Benz Aibuka, Afunguka Mazito …Baada ya Kuacha Kutumia Madawa ya Kulevya

0
Mwanamuziki Rashid Makwiro ‘Chid Benz’ .

 STORI: BONIPHACE NGUMIJE, RISASI JUMAMOSI, HABARI

DAR ES SALAAM: HUYU HAPA! BAADA ya Mwanamuziki Rashid Makwiro ‘Chid Benz’ kupotea kwa muda mrefu kwenye gemu la Muziki wa Bongo Fleva, kufuatia kutopea kwenye matumizi ya madawa ya kulevya, hatimaye ameibuka na kufunguka mambo kibao.

Akizungumza na Risasi Jumamosi hivi karibuni, Chid Benz ambaye kwa sasa yupo jijini Dar akitokea Zanzibar alikokuwa amekwenda mapumzikoni baada ya kutoka mkoani Iringa alikokuwa kwenye kituo cha kusaidia waathirika wa madawa ya kulevya, amesema kwa sasa yupo fiti kiafya na kiakili na anachowaza ni muziki na maisha tu.

Hatarudia madawa Chid Benz aliendelea kufunguka kuwa anamshukuru Mungu kwa kumsaidia mpaka amefanikiwa kutoka ‘kuzimu’ kutokana na matumizi ya madawa ya kulevya na kwamba hawezi kurudi nyuma wala kuthubutu kurudia kutumia dawa hizo za kulevya.

“Kwanza sipendi kuzungumzia maisha niliyopitia nyuma. Kwa sasa nahitaji kuzungumzia muziki tu. Lakini kwa kifupi namshukuru Mungu kunitoa nilikokuwa na kunifanya mtu mwingine. Wakati ule nilikuwa sihitaji hata kuonana na watu kutokana na muonekano wangu lakini kwa sasa ninaonana na kila mtu,” alisema Chid Benz.

Amerudi nyumbani kwao Chid aliendelea kuongeza kuwa, tofauti na wakati wa nyuma alipokuwa anaishi mitaani kwenye ‘mageto’ ya washikaji zake, kwa sasa amerudi nyumbani kwao na anaishi na familia yake na maisha yametawaliwa na furaha.

“Wakati natumia dawa za kulevya nilikuwa naishi kwenye mageto ya washikaji mitaa ya Kinondoni, sikuhitaji kukaa nyumbani kwa sababu mazingira hayakuwa r a f i k i k w a n g u katika kutumia madawa hayo,” alifunguka Chid na kuongeza kuwa; “Mama yangu kwa sasa anafuraha sana, lakini nina mpango wa kuiunganisha familia yangu pamoja, namaanisha watoto wangu ingawa katika hili naomba niishie hapa, nisiingie ndani zaidi maana si vizuri kuzungumza kila kitu.”

Alipokuwa Zanzibar alifanya nini? Akifunguka kuhusu maisha yake ya Zanzibar, Chid Benz alisema kuwa kikubwa ilikuwa ni kupumzika na kutumia muda mwingi kufikiria maisha yake, alikotoka na anakoelekea. Tofauti na hivyo alisema alikuwa anatembelea studio za washikaji zake wa zamani ambao alikuwa nao karibu kabla hajaingia kwenye matumizi hayo ya madawa ya kulevya. Kapika dude na Q-Chillah “Nimeingia studio pale Kill Records na kufanya kazi na mkongwe mwenzangu Q- Chillah ambayo itatoka soon.

Menejimenti yangu inajipanga kwa sasa juu ya kufanya video kali na kila kitu kikikamilika nitaachia ngoma hewani,” alisema Chid Benz.

Hata hivyo alipoulizwa juu ya nani anayemsimamia katika kazi zake kwa sasa Chid Benz hakutaka kuweka wazi kwa kudai kuwa, ana sababu maalumu za kufanya hivyo. Alipoulizwa kuhusu kufanya kazi na msanii mwenzake Shetta kutokana na video iliyoonekana kwenye mitandao ya kijamii wakiwa pamoja, Chid alisema: “Shetta ni mdogo wangu. Tulikutana tu na tukafurahi na kurekodi kile kividio, lakini hakuna kitu chochote kati yetu ambacho kinaendelea kama kazi ikiwepo nitafunguka pia.

Kila kitu kwenye maisha yake ni miujiza Chid alimalizia kwa kusema kuwa, kila kitu katika maisha yake ni mfano wa miujiza ama muvi na haamini kuwa ameweza kufanikiwa kuachana na unga na kuwa mtu safi. “Ni jambo la kumshukuru Mungu. Ilikuwa ni vigumu kuamini kuwa ningeweza kurudi kama nilivyo leo n a kumiliki tena usafiri na maisha yakasonga mbele, niseme tu mambo ya nyuma yamepita na sasa ninasonga mbele tu,” alimaliza Chid.

Leave A Reply