The House of Favourite Newspapers

Dhamana ya Lema Bado Ngoma Nzito na Leo Imekwama, Kula Mwaka Mpya Gerezani

lema

ARUSHA: Mahakama Kuu Kanda ya Arusha iliyokuwa isikilize leo kesi ya rufaa ya Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema (CHADEMA), ya kupinga kunyimwa dhamana imeshindwa kusikilizwa kufuatia upande wa jamhuri kukata rufaa ya kupinga kuongezwa muda wa notisi ya rufaa kwa mbunge huyo.

Kufuatia kukwama kusikilizwa kwa rufaa hiyo, Mbunge Godbless Lema amerejeshwa rumande katika gereza la Kisongo, Arusha hadi Januari 2, 2017 kesi yake itakapotajwa tena.

Maamuzi ya dhamana ya Mbunge Godbless Lema yatatolewa Januari 4, 2017 baada ya jaji kufanya majumuisho ya rufaa za pande zote mbili Januari 2, 2017.

Tujikumbushe

Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, ililikubali ombi la  Mbunge Godbless Lema,  la kuongezewa muda wa kuwasilisha Notisi ya nia ya kukata rufaa ya dhamana yake.

 Akitoa uamuzi wake mnamo Desemba 20, mwaka huu, Jaji Dk. Modesta Opiyo wa Mahakama hiyo, alisema Mahakama hiyo imeruhusu maombi ya kuwasilisha Notisi ya kuomba kuongezewa muda wa kuwasilisha notisi ya nia ya kukata rufaa ya dhamana yake.

Lema anakabiliwa na kesi hiyo ya uchochezi aliyosomewa katika Mahakama ya Wilaya ya Arusha mbele ya Hakimu Mkazi Deusdedit Kamugisha, Novemba 8, mwaka huu na aliwekewa pingamizi na mawakili wa serikali ya kutopata dhamana baada ya hakimu kusema kuwa dhamana iko wazi.

Mbunge huyo wa Arusha Mjini alikamatwa Novemba 2, mwaka huu mkoani Dodoma kwa kosa hilo baada ya kuhutubia katika mikutano ya hadhara katika kata mbalimbali za Jiji la Arusha kuwa ameoteshwa kuwa Rais Magufuli atakufa kabla ya mwaka 2020, hali inayodaiwa kuleta uchochezi kwa wananchi waliomchagua kuwa rais wa nchi.

Comments are closed.