Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Isdor Mpango akiambatana na Mkewe Mama Mbonimpawe Mpango hii leo Agosti 4, 2021 amefika nyumbani kwa aliyekuwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Elias John Kwandikwa Kibaha Picha ya Ndege ili kuwapa pole na kuwafariji wanafamilia kufuatia kifo cha Waziri huyo.
Makamu wa Rais ameweka saini katika kitabu cha maombolezo na baadaye kuzungumza na Mke wa Marehemu Bi.Mareceline Kwandikwa Ambapo amempa pole na kumuomba kuwa na moyo wa subira katika kipindi hiki kigumu.
Baadaye akizungumza na waombolezaji waliojitokeza nyumbani hapo, Makamu wa Rais amemtaja Marehemu Elias Kwandikwa kama kiongozi aliyekuwa na sifa za kipekee. Amesema marehemu Kwandikwa alikua mcha Mungu, Mpole , Mtulivu na mtu aliefanya kazi kwa uwezo wake wote. Amewataka waombolezaji kuendelea kuwa na moyo wa subira na kuwaombea faraja familia ya marehemu Elias Kwandikwa.