The House of Favourite Newspapers

Hakimu wa Kabendera Ateuliwa Kuwa Jaji, Kesi Yakwama

KESI ya uhujumu uchumi inayomkabili Mwandishi wa Habari, Erick Kabendera imeahirishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu hadi Novemba 20, 2019 baada ya hakimu aliyekuwa akiisikiliza, Augustine Rwizile kuteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama Kuu.

 

Kabendera katika kesi hiyo anakabiliwa na mashtaka matatu likiwamo la utakatishaji wa zaidi ya Sh173 milioni.

 

Wakili wa Serikali Mwandamizi, Wamkyo Simon leo Alhamisi Novemba 7, 2019 amedai mbele ya Hakimu Mkazi Vicky Mwaikambo kuwa kesi hiyo ilipangwa kutajwa na upelelezi haujakamilika.

 

Wankyo ameeleza kuwa Rwizile ameteuliwa kuwa jaji na kuiomba mahakama hiyo kuahirisha kesi hiyo wakati wakisubiri ipangiwe hakimu mwingine wa kuisikiliza.

 

Baada ya kusikiliza hoja hiyo, Hakimu Mwaikambo aliiahirisha kesi hiyo hadi Novemba 20, 2019 kwa ajili ya kutajwa.

 

Katika shtaka la kwanza, Kabendera anadaiwa kuwa alijihusisha na mtandao wa kihalifu kwa kutoa msaada kwa genge la uhalifu kwa nia ya kujipatia faida.

 

Shtaka la pili anadaiwa kuwa bila sababu, alikwepa kodi ya Sh173,247,047.02 ambayo ilitakiwa ilipwe Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

 

Katika shtaka la tatu, Kabendera anadaiwa kutakaisha Sh173,247047.02 huku akijua fedha hizo ni zao la kujihusisha na genge la uhalifu na utakatishaji fedha.

 

Comments are closed.