The House of Favourite Newspapers

Hali 4 za kihisia zinazoweza kukwamisha malengo yako!

0

Ulishawahi kukaa na kujiuliza ni jinsi gani hisia zako zinaweza kukusukuma ukafanya jambo ambalo hukulitegemea? Huenda hujajiuliza lakini nikwambie tu kuwa hisia ni adui mkubwa wa maendeleo ya binadamu hasa kama utashindwa kuzizuia zisiathiri maisha yako.

Kisaikolojia inaelezwa kuwa, wakati mwingine hisia ni adui kwa sababu huweza kukudumbukiza kwenye anasa na hatimaye kujikuta unakwama kwenye kutimiza malengo yako. Wiki hii nitaelezea hali za kihisia ambazo zimewafanya wengi washindwe kufikia malengo yao.

1. Furaha iliyopitiliza
Hali hii inapokutokea hujiona ni mtu unayeweza kufanya lolote lakini pia unaweza kujikuta unashindwa kufikia malengo mazuri uliyojipangia.

Mfano: Unadhani ni kwa nini kwenye mabaa na kasino wanatumia muziki mkubwa na kunakuwa na kelele nyingi? Hii yote ni ili kukufanya upate hisia ya furaha inayoweza kukusukuma kutumia mshahara wote hapo baa.
Hii ni kwa sababu kwa wakati huo una furaha kupitiliza kutokana na mazingira hayo, unajikuta unasahau malengo yako na hata shida za nyumbani.
Ukitaka kuamini hili, kumbuka wenzako ambao wamewahi kuchukua mkopo na kwenda nao baa, huwa wanafurahi, anaanza kwa kujinunulia yeye na watu alioongozana nao, furaha ikizidi anaanza kugawa pombe kila meza akiamini ana hela nyingi kumbe zile pesa ni kwa ajili ya matumizi yaliyomfanya achukue mkopo.

2. Wasiwasi
Hii ni hisia nyingine mbaya ambayo inaweza kukusababishia ukaharibu mali zako na hata maisha kwa ujumla.
Wasiwasi katika maisha ya binadamu wakati mwingine husaidia lakini wakati mwingine huharibu mambo kabisa.
Unaweza kuwa unataka kufanya mabadiliko labda ya ofisi yako kwa kutumia fedha nyingi lakini usifanye lolote tu pale hali ya wasiwasi itakapokuingia kwani unahisi huenda ukiitumia fedha haitarudi. Huyu ni adui mkubwa na hakika huwezi kufikia malengo yako kama utakuwa ni mtu mwenye wasiwasi kila wakati.
Utakuta mtu anataka kufungua duka lakini anashindwa kwa kuhofia kuwa atakosa wateja na hela alizoziandaa kufungulia duka zikaenda bure, ‘huyu wasiwasi’ bado atakuwa ni adui kwa sababu hakupi nafasi ya kufanya jambo kwanza.

3. Huzuni
Inadaiwa ukiwa na huzuni mara nyingi uwezo wa kufikiria na kupanga malengo huwa ni mdogo sana.
Hivi hujawahi kuona ukiwa na huzuni unatamani kulala tu au kwenda baa kukutana na watu, ingawa wengine huwa hawapendi hata kukutana na watu?

4. Hasira na kuhisi kuonewa
Hisia hizi ni hatari zaidi ya zote kwani kama usipokuwa mwangalifu unaweza kujikuta unafanya jambo ambalo si zuri kabisa, ukajihatarishia maisha yako na hata ya familia yako kwa ujumla.
Unaambiwa ukiwa na hasira usimtumie ujumbe wa sms mtu aliyekuudhi au usiongee mbele za watu maana unaweza kujikuta unadharaulika kwa maneno utakayoyatoa.
Ndiyo maana unashauriwa kutuliza hisia zako kwanza kabla ya kufanya jambo lolote linaloyahusu maisha. Kamwe usiruhusu hisia zikatawala maisha yako.
Kibinadamu huwezi kuishi bila kupatwa na hisia hizo lakini kikubwa cha kufanya ni kuhakikisha unazituliza ili zisije zikakuletea madhara.
Ukihisi una furaha nyingi kaa mbali na pesa zako, ukiwa na huzuni jaribu kuwa karibu na watu wanaoweza kuipoteza kama siyo kuipunguza hali hiyo, ukiwa na wasiwasi pia washirikishe watu waliowahi kupitia mambo hayo watakushauri pia, lakini ukiwa na hasira fanya kila uwezalo kuzipunguza ikiwa ni pamoja na kunywa maji mengi.

Leave A Reply