The House of Favourite Newspapers

Hawa: Diamond Mungu Atakulipa

MSANII wa muziki ambaye aliwahi kuwa mwandani wa Mbongo- Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’, Hawa Mayoka ‘Hawa wa Nitarejea’ amemfungukia staa huyo na kusema Mungu atamlipa kwa kile alichomfanyia.

 

Akizungumza na Ijumaa Wikienda, Hawa alisema kitendo cha Diamond kujitolea kumsaidia matibabu ya kumpeleka nchini India kimemliza mno kwa sababu hakujua kama ipo siku angemkumbuka.

 

“Nilivyosikia Diamond ameamua kunisaidia nilijisikia furaha mpaka machozi yakawa yananitoka maana sikuamini, Mungu atamlipa na namuombea azidi kuwa na moyo huohuo.

“Nilishakata tamaa kabisa ya kupata matibabu kutokana na uwezo wa kifedha kuwa mdogo kwani madaktari wa hapa walisema natakiwa kutibiwa India, kwa sasa nimepata tumaini jipya baada ya Diamond kujitolea kunipeleka kwenye matibabu India,” alisema Hawa.

 

Kwa upande wa mama yake Hawa, Ndigina Said alisema kuwa hana cha kumlipa Diamond maana amefanya kitu kikubwa kwa mtoto wake hivyo ni Mungu pekee anayeweza kumlipa.

“Yaani hapa sijui nianzie wapi kushukuru ila Mungu tu ambariki Diamond maana naona kabisa anaenda kuokoa maisha ya mwanangu,” alisema mama huyo.

 

Hivi karibuni Diamond alijitolea kumsaidia Hawa matibabu nchini India ambayo yatagharimu shilingi milioni 50 ikiwa ni baada ya kuugua kwa muda mrefu akisumbuliwa na ugonjwa wa ini.

Akithibitisha taarifa za msaada huo wa matibabu, Pili Misana ambaye ni mmiliki wa kituo cha kuacha matumizi ya madawa ya kulevya kinachojulikana kama Pillimissana Foundation kilichopo Kigamboni, Dar alisema ni kweli Diamond ameamua kumpeleka Hawa India na ameshatafuta na daktari wa kumtibia hivyo kuna taratibu kidogo zinakamilishwa ndipo asafiri.

 

“Tunamshukuru sana Diamond na Babu Tale (meneja wa Diamond) wameamua kujitoa kumtibia Hawa na tayari ameshamtafuta daktari siku za hivi karibuni atasafiri na matibabu yatagharimu shilingi milioni 50 na yeye ndiye atakayegharamia,” alisema Pili.

STORI: Imelda Mtema, DAR

Diamond Platnumz Afunguka Tatizo la Hawa wa Nitarejea

Comments are closed.