The House of Favourite Newspapers

Hersi Athibitisha Kuwakabidhi Mil 300 Nyota Yanga

0

Ni rasmi sasa ile zawadi ya Sh milioni 300 ambayo mabosi wa Yanga waliwaahidi wachezaji na benchi la ufundi la timu hiyo pindi watakapotwaa taji la Mapinduzi kwa kuifunga Simba katika mchezo wa fainali, inatarajiwa kukabidhiwa leo Jumatatu.

 

Taarifa kutoka ndani ya Yanga zinaeleza kuwa Yanga iliahidiwa kitita cha Sh milioni 200 kabla ya kuchezwa kwa fainali hiyo lakini baada ya kufanikiwa kuifunga Simba mikwaju ya penalti 4-3, mabosi pamoja na viongozi wa Yanga waliongeza milioni 100 nyingine na kufika kiasi cha milioni 300.

Akizungumza na Championi Jumatatu, Mkurugenzi wa Uwekezaji wa GSM na Mwenyekiti Msaidizi wa Kamati ya Usajili Yanga, Eng. Hersi Said, alisema kuwa Jumatatu watahakikisha wanawapatia fedha zao wachezaji wote na benchi la ufundi ambalo kwa pamoja walifanikiwa kuipa ushindi timu hiyo.

 

“Tunatambua mchango mkubwa wa wapambanaji wetu ambao wametupa heshima kubwa ya Kombe la Mapinduzi, kama watu wataliona hili ni kombe dogo basi watambue baada ya hili makubwa mengine yatakuja kupitia hawahawa wapambanaji wetu.“

 

Kwa kuutambua mchango wao kwetu, naomba niwaahidi kuwa Jumatatu wachezaji wote na benchi la ufundi watapata ile zawadi ya ahadi tuliyowaahidi, hivyo niwahakikishie kuwa wachezaji wetu wataendelea kufurahi kama watazidi kuwaletea ninyi wananchi furaha, ambayo ni makombe,” alisema kiongozi huyo.

Stori: Marco Mzumbe, Dar es Salaam

#LIVE: DIAMOND ANAVUNJA UKIMYA, ANAZUNGUMZA NA WANAHABARI MUDA HUU…

Leave A Reply