The House of Favourite Newspapers

Jeshi la Polisi Lawataka Madereva Kutokuwa Chanzo cha Huzuni na Majonzi

0

 

 

Jeshi la Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani nchini kimesema zipo sheria zinazotoa miongozo na taratibu za matumizi sahihi ya barabara hapa nchini huku likiwataka madereva kutokuwa chanzo cha huzuni kwa Watanzania kwa kusababisha ulemavu wa kudumu na kupoteza maisha ya watanzania.

Hayo yamesemwa mapema leo, Desemba 23, 2023 na Afisa Mnadhimu Namba Moja wa Kikosi cha Usalama Barabani Nchini, Kamishna Msaidizi wa Polisi, ACP Pili Misungwi katika kituo cha mabasi yaendayo mikoani na nchi jirani jijini Arusha ambapo amebainisha kuwa kikosi hicho kinaendelea na oparesheni zake za ukaguzi na kutoa elimu nchi nzima lengo likiwa ni kutomeza ajali hapa nchini.

ACP Misungwi ameeleza kuwa hivi karibuni kikosi hicho kilifanya uhakiki wa leseni nchi nzima ili kubaini madereva wenye sifa ambao wanapaswa kuendesha vyombo vya moto huku akibainisha kuwa kwa sasa wanahakiki madereva hao kama wanasifa za kuendesha vyombo husika hapa nchini.

Pia amewataka abiria kote nchini kupaza sauti kwa baadhi ya madereva wanaokiuka sheria za usalama barabarani na pale inapobidi kumwambia dereva asiendeshe kwa mwendo kasi ikiwa ni pamoja na kutoa taarifa kwa Jeshi la Polisi ili hatua stahiki zichukuliwe kwa dereva ambaye amekiuka sheria za usalama barabarani.

Afisa mnadhimu huyo ametumia fursa hiyo kuwatakia safari njema abiria wanaosafiri kwenda maeneo tofauti tofauti hapa nchini na nje ya nchi heri ya Krismasi na mwaka mpya 2024.

Nao baadhi ya abiria wanaokwenda maeneo tofauti tofauti hapa nchini wamesema operesheni hiyo imekuja wakati sahihi ambapo kipindi hiki wananchi wengi wanakwenda maeneo mbalimbali hapa nchini kusalimia ndugu na jamaa huku wakilipongeza Jeshi la Polisi hususani Kikosi cha Usalama Barabarani kwa kuendelea kutoa elimu na kufanya oparesheni hizo ambazo zimesaidia kupunguza ajali nchini.

Amini Khamis ambaye ni dereva wa basi la Kampuni ya Hajjis, amesema wao kama madereva wanaendelea kufuata sheria za usalama barabarani ambazo zinawaongoza huku akibainisha kuwa elimu waliyopewa na afisa mnadhimu namba moja wa kikosi cha usalama Barabarani nchini yote waliyoambiwa watayafanyia kazi.

Leave A Reply