Kampeni Ya Rais Dk. Samia Yazidi Kuungwa Mkono, Oryx Gas Yafikisha Huduma Ya Kisasa Soko la Feri
NAIBU SPIKA wa Bunge Hassan Zungu, amewahakikishia Mama Lishi na Baba lishe katika Soko la Samaki la Kimataifa Feri kuwa watafungiwa mtambo wa nishati safi ya kupikia ili kuwaepusha kutumia fedha nyingi kununua gesi kupitia mitungi midogo.
Amesema hatua hiyo ni utekelezaji wa ]mkakati wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa lengo la kulinda mazingira kuwaweka wanawake katika nafasi nzuri ya kujiendeleza kiuchumi.
Zungu alitasema hayo jana sokoni hapo, jijini Dar es Salaam wakati wa kugawa mitungi 200 kati ya 700 iliyotolewa kwa Mama na Baba lishe hao ambayo imetolewa kwa ushirikiano wa Zungu na kampuni ya Gesi ya Oryx Tanzania.
Naibu Spika Zungu ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Ilala, alitoa ahadi hiyo baada ya kupokea maombi ya wafanyabiashara hao kupitia kwa kiongozi Zone Namba 7 katika soko hilo, Said Mpinji aliyelalamika kuwa wanalazimika kutumia sh. 110,000 kila siku kujaza gesi ya kuendeshea shughuli za baba na mama lishe.
Akijibu kilio hicho, Zungu alisema ni cha muda mrefu na kwamba tayari amezungumza na kampuni ya Gesi ya Oryx Tanzania kupitia kwa Mkurugenzi Mkuu wake, Benoit Araman ambaye amekubali kufunga mifumo ya gesi ya kisasa kasha kusambaza huduma hiyo kwa wafanyabiashara hao kwa gharama nafuu.
“Mkombozi wetu ni Rais DkSamia Suluhu Hassan ambaye alianzisha kampeni ya Nishati safi ya kupikia, kuhakikisha Watanzania wanaishi maisha mazuri.
“Oryx wamekubali kuweka mtungi mmoja mkubwa na mifumo ya usambazaji, kasha watasambaza huduma kwa mama na baba lishe waliopo hapa na kuwafungia mita halafu watakuwa wakilipia huduma kama wanavyofanya katika umeme,” alisema.
Kwa upande wake Benoit alisema Oryx wamewafikia wajasiriamali hao kwa lengo la kutekeleza mkakati wa Rais Dk. Samia wa matumizi ya nishati safi ya kupikia kulinda mazingira na afya za wananchi.
Alisema kuwa tangu Julai mwaka 2021, walianza mkakati huo baada ya Rais Samia kutangaza kwamba serikali yake inataka kuona hadi mwaka 2030 asilimia 80 ya Watanzania wawe wanatumia nishati safi ya kupikia.
Mwenykiti wa CCM Mkoa wa Dar es Salaam Abbasi Mtemvu aliyekuwa mgeni rasmi katika hafla hiyo, alisema kilichofanyika ni utekelezaji wa Ilani na kumpongeza Zungu kwa namna anavyowatetea wananchi katika jimbo lake.
“Zungu ni mfano wa kuigwa, amefanya makubwa. Nimekuwa naye bungeni kwa miaka 10 muda wote ameonyesha dhamira ya kutetea wananchi wa jimbo lake, anastahili pongezi,” alisema.
Aliipongeza serikali kwa kuendelea kupeleka maendeleo kwa wananchi huku akiwataka mama na baba lishe wa sokoni hapo kujiandaa kupokea mitaji kutoka serikali ili kunua biashara zao.
Mtemvu alieleza kwamba serikali imetenga sh. bilioni nane kwa mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na halmashauri, na kwamba japokuwa ilisimama lakini muda si mrefu itaanza kutolewa tena.
“Serikali ya CCM ipo tayari kukupeni mitaji kwa kuwa imejiopanga vizuri, sasa jiandaeni kuchangamkia fursa. Aprili mwaka huu utaanza ujenzi mkubwa wa barabara zaidi ya kilometa 200 ambapo zaidi y ash bilioni 188 zitatumika, hii ni fursa kwa mama na baba lishe kupeleka chakula chenu kitamu na kujiingizia kipato,” alisema.