The House of Favourite Newspapers

Kampuni Inayonunua Mkojo wa Wajawazito Kuchunguzwa

0

Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) imesema haiitambui wala haijawahi kuipatia usajili kampuni ya Polai (Tz). Co Ltd kukusanya mikojo ya wajawazito, kwa maelezo kwamba wanaitumia kutengeneza tiba ya magonjwa ya binadamu.

 

TMDA imesema kuwa imeshatoa maelekezo kwa meneja wa mamlaka hiyo kanda ya mashariki kuanza mara moja kuifuatilia kwa ukaribu kampuni hiyo na pindi uchunguzi ukikamilika na kuthibitisha makosa yao, watatoa taarifa kwa umma kuhusu hatua watakazochukua kwa mujibu wa sheria.

 

Mikojo hiyo hukusanywa na huwekwa kwenye vikopo kisha kupelekwa kwenye nyumba iliyopo Mtaa wa Mferejini, Manzese, kabla ya kupelekwa kwa raia wa kigeni anayetajwa kuwa mmiliki wa kampuni hiyo iliyopo Mikocheni jijini Dar es Salaam.

 

Kampuni hiyo ilieleza kuwa ndani ya mikojo hiyo kuna homoni aina ya `human chorionic gonadotropin (HCG), `human menopausal gonadotrophins’ (HMG) na `urokinase’ ambazo ndizo hutumika kutengeneza dawa za matatizo ya ugumba na kiharusi.

 

Mkurugenzi wa dawa na vifaa tiba kutoka TMDA, Akida Khea alisema mamlaka hiyo haiitambui kampuni hiyo na ndio mara ya kwanza wanasikia kuwa kuna mtu anakusanya mikojo ya wajawazito kwa ajili ya kutengeneza dawa.

 

Alisema wao wanafahamu kuwa ni kweli kwenye mikojo ya wajawazito kuna homoni zinazotumika kutengeneza dawa, lakini hawajawahi kusikia njia hiyo inayotumiwa na kampuni ya Polai.

 

“Ili kuweza kujua hawa watu wamepewa kibali cha kuyafanya hayo wanayoyafanya, tumeshatoa maelekezo kwa meneja wa TMDA kanda ya Mashariki aanze mara moja kufuatilia suala hilo kwa ukaribu ili kuweza kujua kwa undani zaidi.

 

“Tukishamaliza na kuthibitisha hayo wanayoyafanya tutatoa taarifa na kueleza watachukuliwa hatua gani kwa mujibu wa sheria,” aliongeza Khea.

 

Hata hivyo, Khea amelishukuru gazeti la Mwananchi kwa kuibua tatizo hilo na kusema kuwa kila mwananchi ata hivyo Khea amelishukuru gazeti la Mwananchi kwa kuibua tatizo hilo na kusema kuwa kila mwananchi anajukumu la kuilinda nchi yake.

 

“Tunashukuru sana kwa kuweza kuibua ishu hiyo kwa sababu mlinda nchi ni mwananchi mwenyewe, kama unavyofahamu sisi hatupo kila mahali hapa nchi hivyo tunategemea pia taarifa kutoka kwa watu, niseme tu stori ni nzuri na tumeanza kuifanyia kazi,” alisema

Leave A Reply