The House of Favourite Newspapers

Katibu Mkuu CCM Awashangaa Katavi Kuendekeza Kamchape

0
KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) Daniel Chongolo amewataka wananchi wa Mkoa wa Katavi kuachana na imani za kishirikina maarufu kwa jina la Kamchape kwani ni chanzo cha uasikini.
Chongolo ameyasema hayo leo Oktoba 2,2023 wakati akizungumza na wananchi na wana CCM baada ya kuwasili Mpanda ambako atakuwa na ziara ya kukagua utekelezaji wa Ilani ya CCM sambamba na kutatua kero za wananchi.
“Nimeambiwa huku kuna kamchape , hawa jamaa mnawapa nguvu kubwa , mnawapa kichwa , mnawapa fursa ya kufanya mambo yanayokiuka sheria za nchi
“Imani za kishirikina ni umasikini na ukitaka kujifunza angalia watu wanaonamini katika ushirikina uone maisha yao.Wanaamini katika ndoto ambazo kutekelezeka kwake ni ngumu.
“Achaneni na kuendekeza mambo yanayoleta taaswira ya umasikini kwa. Mkoa wa Katavi ni mkubwa na mmeshajenga historia kubwa ,huu ni mkoa wa Mhandisi Kamwelwe, Mkoa wa Waziri Mkuu mstaafu Mizengo Pinda, ni mkoa wa watu wazito katika nchi hii,”amesema.
Chongolo amesema haiwezekani mpaka leo Mkoa wa Katavi kuendekeza ushirikina kama daraja la kufanikiwa katika mambo yao , hivyo ni lazima watoke katika kufikiri mambo kirahisi.
Amesisitiza maendeleo hayapatikani kwa ndumba, kwa kupuliza, kwa kuagua , kupiga ramli na kutengeneza mambo rahisi bali maendeleo ni mambo yanayotaka kufuata utaratibu.
“Ukiona watu wa namna hiyo wewe usipate shida angalia maisha yao, mtu anaweza kuwa na ng’ombe 1000 lakini anakula nyama nusu kilo kwa wiki, sababu ya masharti.Achaneni  na maisha hayo , afadhali uwe na ng’ombe 10 lakini uwe na uhuru wa kula nyama.
“Ni afadhali uwe na shamba heka tatu lakini uwe na uhuru wa kula mchele wako, achaneni na mila potofu , mila potofu zinawagombanisha , mila potofu zinawatenganisha…
“Mila potofu zinawatengenezea uadui usio na maana , zinawakwamisha kwenye shughuli za maendeleo.Akija mtu kapiga kamchape yake akawaambia ukilima shamba hili  hutavuna mwaka huu, unaacha kwasababu unaamini alichosema.”
Leave A Reply