The House of Favourite Newspapers

Kilimanjaro Premium Lager Marathon 2021 Yazinduliwa Jijini Dar

0
Mkurugenzi Msaidizi wa Michezo katika Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Alex Nkenyenge aliyemuwakilisha mgeni rasmi Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na  Michezo, Ally Possi akizungumza kwenye uzinduzi huo.

IJUMAA Novemba 13, 2020, msimu  wa 19 wa mbio  maarufu za Kilimanjaro Premium Lager Marathon 2021  umezinduliwa  jijini Dar es Salaam huku  Serikali ikimwagia  sifa  mbio   hizo  kutokana  na  mchango wake   katika   ukuaji wa sekta ya Utalii na uchumi kwa ujumla .

Akizungumza  katika  hafla iliyofana ya uzinduzi  huo uliofanyika  Hoteli  ya  Slip Way jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Msaidizi wa Michezo katika Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Alex Nkenyenge aliyemuwakilisha mgeni rasmi Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na  Michezo, Ally Possi alisema  mbio za Kilimanjaro Premium Lager Marathon zimechangia kwa kiwango  kikubwa ukuaji wa sekta ya utalii wa michezo nchini hivyo kupelekea kuongezeka pato la fedha za kigeni.

Kaimu Katibu Mkuu wa Chama Cha Riadha Tanzania, Ombeni Zavala akisisitiza jambo.

“Tukio hili ambalo huvutia zaidi ya wageni 25,000 katika mji wa Moshi ambao baadhi yao ni washiriki na  watazamaji ambao pia hufurahia vivutio  mbalimbali vya kitalii na kupromoti shughuli  nyingine za kiuchumi katika  mji huu,” alibainisha.

Nkenyenge amewataka wafanyabiashara si tu kuchangamkia fursa zinazoletwa na mbio hizo kwa kutengeneza faida, bali pia   wahakikishe wanatoa huduma na kuuza  bidhaa zenye ubora.

Meneja wa  bia  ya  Kilimanjaro na kinywaji cha Grand Malt, Irene Mutiganzi akizungumza kwenye uzinduzi huo.

Aidha ametoa wito kwa waandaaji wa  mbio nyingine za marathoni nchini   kufuata nyayo za mbio za Kilimanjaro Marathon ambayo imekuwa ikizingatia miongozo ya IAAF na Riadha Tanzania (RT) hivyo kupelekea kukua mwaka  hadi mwaka na kuvutia wadhamini na washiriki kutoka ndani na nje ya nchi.

“Serikali itaendelea kushirikiana na waandaaji wa Kilimanjaro Marathon kuifanya iwe bora na bora,” alisema.

Kuhusiana na janga la gonjwa la Covid-19, Nkenyenge alisema serikali itahakikisha kwamba wale wote wanaohudhuria wanapimwa, haswa wale kutoka nje ya nchi.

Wadau wakifuatilia tukio la uzinduzi.

“Washiriki wa mbio za Kilimanjaro marathoni hawapaswi kuwa na wasiwasi kwa kuwa tutachukua tahadhari zote muhimu katika sehemu zote za kuingilia nchini,” alisema.

Aidha aliwapongeza wadhamini wa mbio za Kilimanjaro ambao wanaongozwa  na Kilimanjaro Premium Lager ambao   ndio wenye dhamana ya mbio za 42km, Tigo-21km, Grand Malt-5km, pamoja  na wadhamini wa meza za maji, Absa Tanzania, Unilever, TPC Limited, Tanga Cement, Kilimanjaro Water na GardaWorld Security, Keys Hotel, Kibo Palace Hotel na CMC Automobiles

Kwa  upande  wake  Meneja wa  bia  ya  Kilimanjaro, Irene Mutiganzi ambaye  pia ni meneja wa kinywaji cha Grand Malt, alisema wanajivunia kuwa wadhamini wa mbio hizo kwa mwaka  wa 19 mfululizo sababu bidhaa zao kujikita kutangaza na kukuza utalii na  utamaduni wa Tanzania kwa ujumla  wake.

Aidha alisema wamejiandaa vizuri kwa  ajili ya mbio za mwakani ambapo  wametenga shilingi milioni 25 kwa ajili  ya zawadi za washindi wa kwanza kwa  mbio hizo kwa upande wa wanaume  na wanawake ambapo washindi watajinyakulia shs milioni 4 kila mmoja na kwa Mtanzania mwanaume na mwanamke wa kwanza watapata shs milioni 1.5 kila mmoja kama motisha.

Mwakilishi wa Baraza la Michezo Tanzania, Kilindi Maona akizungumza na wageni waalikwa.

Hivyo amewataka washiriki kujisajili  kushiriki katika mbio hizo kwa kwa wakati kwani tayari usajili  umeshafunguliwa   rasmi kupitia njia ya mtandao wa  www.kilimanjaromarathon.com  pamoja  na Tigo Pesa kwa kupiga nambari   *149*20#.

Aidha Irene pia amewataka wale ambao watapenda kushiriki kwenye  mbio za kilometa 5 nao wajisajili mapema kwani nafasi za ushiriki zitakuwa  chache kwa mara nyingine tena. Mwaka  huo waandaji walilazimika kufunga  usajili mapema kwani nambari zote  kwenye mbio zote za 42km, 21km na 5km zilikuwa zimeuzwa mapema.

Mkurugenzi Msaidizi wa Michezo katika Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Alex Nkenyenge (katikati) akizindua rasmi mbio za Kilimanjaro Premium Lager Marathon 2021 katika Hoteli ya Slip Way, Jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki. Wengine kutoka kushoto ni Katibu Mkuu wa Kamati ya Olympiki Tanzania, Filbert Bayi, mwakilishi wa Baraza la Michezo Tanzania, Kilindi Maona, Meneja wa Bia ya Kilimanjaro Premium Lager, Irene Mutiganzi, Mkuu wa Huduma za Masoko wa Tigo, William Mpinga na Kaimu Katibu Mkuu wa Chama Cha Riadha Tanzania, Ombeni Zavala.

Naye Mkuu wa Huduma za Masoko wa Tigo, William Mpinga alisema, “Kama kampuni ya mawasiliano inayoongoza  nchini ikiwa na mtandao mpana zaidi  wa 4G, tunafurahi na kujivunia kwa mara nyingine tena kudhamini Tigo Kili Half Marathon 2021 kwa mwaka wa sita  mfululizo.”

“Tunawaomba washiriki kujisajili  kwenye mbio na kulipia ada zao  kupitia  Tigo Pesa kwani ni njia rahisi na ya  uhakika na kwa wale wakimbiaji ambo  hawana laini ya Tigo wanaweza kuwaomba marafiki na jamaa zao  kuwasajili. Tunayo matumaini kuwa Tigo Kili Half Marathon 2021 itaendeleza utamaduni wake wa kusheherekea  pamoja na jamii.

Na Katika kuongezea juhudi za Serikali za kuzuia Covid 19 kupitia hatua kali katika maeneo yote ya kuingilia nchini, waandaaji wa mbio za Kilimanjaro Marathon watahakikisha kwamba maafisa wake wote ambao wanashughulikia wakimbiaji wakati wa usajili na siku ya mbio, wanafuata miongozo ya kimataifa na watakuwa  wamevalia vifaa vya kujikinga (PPE)  ikiwa ni barakoa na vitakasa mikono  pamoja na kuhakikisha na kunakuwepo kutotangamana kwa watu (Social distancing) kama moja ya vipaumbele vyao.

Wadau katika picha ya pamoja baada ya uzinduzi.

Hafla ya uzinduzi huo ilihudhuriwa pia na wawakilishi wa Baraza la Michezo la Tanzania (BMT), Kamati ya Olimpiki ya Tanzania (TOC), Riadha Tanzania (RT), vilabu vya mbio na vyombo vya habari.

Kulingana na waandaaji, msimu wa 19 wa mbio za Kilimanjaro Premium Lager Marathon utafanyika Jumapili Februari 28, 2021 katika Chuo Kikuu cha Ushirika cha Moshi (MoCU).                   HABARI/PICHA ZOTE NA RICHARD BUKOS

Leave A Reply