The House of Favourite Newspapers

Kisa Rosa Ree… uhusiano wa Aika, Nahreel watibuka!

0

navykenzoofficialNavy Kenzo

DAR ES SALA-AM: Ule uhusiano uliodumu kwa zaidi ya miaka mitano unaowahusisha wasanii wanaotamba katika Muziki wa Bongo Fleva wakitumia jina la Navy Kenzo, Emmanuel Mkono ‘Nahreel’ pamoja na Aika Mareale unadaiwa kutibuka huku sababu ikimuhusisha msanii wao anayejulikana kama Rosa Ree.

TUJIUNGE NA CHANZO

Kwa mujibu wa chanzo cha karibu na wasanii hao wanaotamba na vibao vingi ikiwemo Aiyola, Game, Kamatia Chini na vingine kibao, kwa sasa wamekuwa kama chui na paka na wapo katika kujutia kwa kumuweka Rosa katika lebo yao ya The Industry.

“Kama inavyojulikana Aika na Nahreel wana lebo kama walivyo wasanii wengine ambapo katika lebo hiyo kuna wasanii wachache akiwemo Rosa. Sasa mbali na kumuweka dada huyo kwenye lebo kumbe Nahreel anatoka naye bila Aika kujua,” kilisema chanzo.

Rosa RobertsRosa Ree.

WAPELEKANA ‘SUPAMAKETI’

Chanzo kinazidi kutiririka kuwa wawili hao wamezidisha ukaribu na hivi karibuni wakati Aika akiwa hayupo nyumbani ambapo Rosa huwepo mara kwa mara kwa ajili ya kurekodi kwa sababu studio na nyumba vipo karibu, Nahreel alitumia upenyo huo kutoka naye.

“Ilikuwa ni kawaida yake kumvizia Aika akiwa hayupo, sasa siku hiyo akapata upenyo na kumuomba Rosa waende naye supamaketi kwa ajili ya manunuzi ya hapa na pale kisha wapitie kwenye mambo yao, kumbuka wakati huo Aika hakupewa taarifa yoyote,” kiliendelea kumwaga ubuyu chanzo hicho.

KIMBEMBE CHAANZA

Inadaiwa walikaa muda mrefu, Aika alifura kwa hasira akiwasubiri kwa hamu maana alikuwa ameshatonywa kila kitu kilichokuwa kikiendelea katika uhusiano huo mchanga.

“Alikuwa akimsubiri Nahreel arudi aweke wazi amchague yeye ama Rosa lakini baadhi ya marafiki wa karibu wa Nahreel walikuwa wakimsihi sana asimfanyie hivyo na asiweke hasira mbele huenda anavyohisi sivyo.”

WAISHI ‘KIBUBUBUBU’

Chanzo bado kinaendelea kumwaga ubuyu kuwa baada ya Nahreel kurudi, Aika alishusha mori, alikuwa ameya-elewa maneno aliyo-kuwa akiambiwa na marafiki wa Nahreel hivyo aliamua kumbadilishia adhabu, kutoka kumuacha hadi kuishi naye kibubububu.

“Si Nahreel wala Aika hakuna aliyekuwa akimuongelesha mwenzake ni kama walikuwa wakiishi kibubububu. Walikaa zaidi ya wiki moja na nusu hakuna aliyetaka kumuongelesha mwenzake na hata Rosa alikuwa amekalia kuti kavu,” kilimaliza chanzo hicho.

AIKA HUYU HAPA!

Amani lilimtafuta Aika kujua ukweli ambapo alikiri kuwepo kwa ugomvi huo na kujitetea kuwa walishayamaliza.

“Ujue mimi na Nahreel tumetoka mbali sana kwa hiyo linapotokea suala la kukorofishana huwa linatokea kwa muda kisha linaisha, kwa sasa nipo naye sawa tu jamani,” alisema Aika.

NAHREEL NAYE ANASEMAJE?

Kwa upande wa Nahreel naye alikubali kutokea kwa mvurugano huo na kusema kuwa kamwe hawezi kuja kumuacha mwandani wake huyo.

“Hapa nilipo nina vidonda vya tumbo hata Aika naye anavyo na hii yote ni kutokana na kushinda na njaa kipindi cha nyuma tukihangaika pamoja kutoka. Nampenda na siwezi kumuacha kwa maana migogoro huwa ipo tu,” alisema Nahreel.

ROSA REE JE?

Rosa alisema kuwa ni kweli alitoka na Nahreel lakini anamchukulia kama meneja wake hawezi kujiingiza katika uhusiano wakati anaelewa kuwa wanaomsimamia ni mabosi zake.

“Vitu kama hivyo huwa vinatokea lakini nashukuru tu vimeisha na maisha yanaendelea.”

AIKA NA NAHREEL NI NANI?

Aika na Nahreel ni moja ya kapo inayokubalika kwa sasa kwenye Muziki wa Bongo Fleva. Wawili hao walikutana miaka mitano nchini India ambapo kila mmoja alikuwa akisomeshwa na wazazi wake. Waliingia katika Kundi la Pah One lililokuwa likiundwa na wakali kama Ola na Igwe ambapo baadaye walikuja kutengana na kuamua kutengeneza kundi lao waliloliita Navy Kenzo.

Leave A Reply