Moto mkali ukiunguza Ofisi za Kliniki ya afya ya mapenzi iliyopo jijini Mwanza leo.
Ofisi hizo zikizidi kuungua kwa moto.
Zimamoto wakijaribu kupambana na moto huo.
Na Idd Mumba, Mwanza
Ofisi za Kliniki ya afya ya mapenzi iliyopo jijini Mwanza karibu na jengo la Nyanza leo majira ya saa tisa alasiri imeungua moto na kuteketeza vitu mbalimbali vilivyokuwepo katika kliniki hiyo.
Wakizungumza na www.globalpublishers.co.tz mashuhuda wa tukio hilo wamesema waliona moshi ukitoka katika ofisi hizo na kutoa taarifa kwa jeshi la zimamoto ambalo liliwahi kufika katika eneo la tukio lakini walitumia muda mrefu kufunga bomba la kurushia maji jambo lililosababisha kuungua kwa vifaa vingi vya ofisi hiyo.
Kwa upande wake, mmiliki wa kliniki hiyo, Paul Nelson amesema wakati tukio hilo linatokea yeye alikuwa Mwanza Hotel iliyopo karibu na ofisi hiyo na aliona moshi mkubwa ukitoka katika ofisi yake na kutoa taarifa kwa zimamoto.
Nelson amesema chanzo cha moto huo kimenatokana na shoti ya jenereta lililokuwa limewashwa kutokana na kukatika kwa umeme na jenereta hilo lilikuwa halitumiki kwa muda mrefu jambo ambalo limefanya kutokea kwa shoti hiyo na kusababisha moto mkali uliounguza ofisi yake.
Alivitaja vifaa vilivyoungua kuwa ni pamoja na laptop yenye thamani ya shilingi laki nane (800,000/=), simu mbili pamoja na mafaili aliyokuwa anayatumia katika ofisi hiyo.