The House of Favourite Newspapers

Kwa hizi kufuru za kijinga, ipo siku Mungu atatuadhibu!

0
love, family, finance, money and happiness concpet - smiling couple with money and piggybank ot table at home
love, family, finance, money and happiness concpet – smiling couple with money and piggybank ot table at home

Ni wiki nyingine tulivu tunakutana tena kupitia ukurasa huu ambapo tunaelimishana na kukumbushana juu ya mambo mbalimbali yanayogusa maisha yetu ya kila siku.

Nichukue fursa hii kumshukuru Mungu kwa kila kitu kwa kuwa amekuwa akiniongoza katika mstari ambao umenyooka. Hata kama wakati mwingine huwa natoka kwenye mstari, hiyo inatokana na udhaifu alionao kila binadamu.

Mpenzi msomaji wangu, hivi karibuni nikiwa maeneo f’lani ya Oysterbay jijini Dar nilishuhudia tukio ambalo lilinitoa machozi. Nilikuwa napita kwenye eneo moja lililokuwa na mapipa ya taka, nikakutana na watoto wawili ambao walikuwa wakiokota chakula.

Mmoja alikuwa na mfuko ambao sikujua ndani yake kulikuwa na nini, mwingine alikuwa ameshika mikate miwili ambayo inavyoonekana waliiokota ndani ya mapipa yale.

Tukio hilo si mara ya kwanza kuliona na naamini hata wewe ulishawahi kushuhudia watu mbalimbali wakiokota vyakula majalalani.

Yawezekana baadhi yao hawana akili timamu lakini nikuhakikishie tu kwamba wapo ambao wana akili zao na wanajua ni madampo gani ya ‘wenye nazo’ wakipita hawakosi vyakula ambavyo walistahili kupewa wao.

Najua zipo familia ambazo zimejaaliwa kuwa na uwezo kiasi kwamba chakula kwao wala siyo jambo la kuumiza kichwa. Stoo kwao kumejaa kila aina ya vyakula, ni wao tu kuamua nini wale kwa siku husika.

Familia hizi ndiyo zile ambazo baadhi yao wanajijua kabisa kilo moja ya mchele hawamalizi lakini watapika na kitakachobaki wanaenda kutupa jalalani. Mikate wanajua kabisa siyo walaji kivile lakini watanunua na kesho yake unaikuta imetupwa kwenye mapipa ya taka.

Watu wanaofanya hivi wanamkufuru sana Mungu! Hivi wewe ambaye unafikia hatua ya kwenda kutupa chakula jalalani hujui kwamba zipo familia zinakufa na njaa? Tena siyo mbali, unaweza kukuta majirani zako wanashindia mlo mmoja lakini kuwasaidia inakuwa ngumu, huu ni ubinadamu kweli?

Najua kama siyo wewe, wapo watu unaowajua ambao wana tabia hii ya kufuja vyakula, wanakula hadi wanasaza lakini hawafikirii zile familia maskini ambazo zinaishi kwenye mazingira magumu. Hii siyo sawa jamani.

Hivi unajisikiaje pale ambapo asubuhi umeenda kutupa kiporo kisha njiani ukakutana na mtoto ambaye anakuomba pesa ili akapate chakula? Hujisikii vibaya? Huoni kwamba kile ulichokitupa ndicho alichostahili kula yule aliyekikosa?

Jamani, Mungu anapokujaalia uwezo wa kuwa na fedha ujue anafanya hivyo kwa makusudi. Anataka utumie pesa zako kuwasaidia wengine ambao hakuwajaalia hicho ulichonacho wewe.

Mungu anajua wapo maskini ambao kuishi kwao kunakutegemea wewe tajiri hivyo kushindwa kwako kuwasaidia na kufuja kile ulichobarikiwa ni kumkasirisha Muumba.

Ukiacha hilo la kufuja vyakula, wapo ambao wana pesa nyingi lakini jinsi wanavyozitumia utashangaa. Badala ya kufanya mambo ambayo yana maana utakuta mtu anazitumia pesa zake kusaka heshima baa. Akienda baa yeye ni kutoa ofa kwa kila anayekatiza mbele yake.

Mbaya zaidi watu hawa hawatoi ofa kwa watu wenye uhitaji. Hata wale ambao wana pesa zao na wameenda baa ili nao wakaoneshe wanazo, nao wanapewa ofa. Huu ni ulimbukeni uliopitiliza!

Hivi utampaje mtu msaada ambao hauhitaji? Hujawaona ambao wanastahili kuzitumia hizo pesa zako za ziada? Tena sasa, wale ambao unawapa ofa za bia hata wakikuambia ‘asante’ hupati baraka yoyote ila ungeenda kumpa maskini mwenye uhitaji, ukamwambia; ‘hii kanunue nguo, hii kanunue chakula, hii kalipie ada za watoto’ shukrani yake itatoka kwa dhati kabisa na hakika Mungu atazidi kukubariki.

Niseme tu kwamba kama umejaaliwa kuwa nacho saidia wale ambao wanastahili kusaidiwa. Hakikisha humchukizi Mungu kwa matendo yako yanayotokana na fedha alizokujaalia. Kama una pesa zinazokusumbua, wapo watoto yatima wanaohitaji msaada wako.

Kama una chakula kingi stoo, huna sababu ya kusubiri kikushinde ukakitupe jalalani kiokotwe na wenye uhitaji, kigawe mapema kwa wasiojiweza. Kumbuka unapotupa chakula, unapotumia pesa katika mambo ya anasa ipo siku Mungu atakuhumu kwa hilo.

Leave A Reply