The House of Favourite Newspapers

Lulu Diva Avunja Ukimya Kutua Wasafi

0

KUTOKA kwenye vichupa vya Bongo Fleva kama Naogopa cha msanii Mirrow, Burger Movie Selfie cha Belle 9 na Pamela cha Barakah The Prince, ndipo sura yake ilipoanza kuonekana akiwa kama video vixen.

Huyu ndiye Lulu Diva au Lulu la Diva. Jina lake halisi ni Lulu Abbas kutoka Tanga moja hiyo!

Mbali na kuuza nyago kwenye video, Lulu Diva ambaye alikuwa Mshiriki wa Miss Pwani mwaka 2015, ameshakimbiza kunako Bongo Fleva na ngoma kama Homa, Chekecha, Ona, Utamu, Mapopo, Amezoea na hii ambayo inatamba kwa sasa Naogopa aliyomshirikisha Mr Blue Byser Babylon.

Kama ujuavyo, biashara ya shoo (showbiz) haiendi bila vikorombwezo. Lulu Diva amekuwa akitrendi na mambo kibao, huku akihusishwa kujiunga na Lebo ya Wasafi na uhusiano wake na lejendari wa Bongo Fleva, Khaleed Mohammed ‘TID Mnyama’ au ‘Mzee Kigogo Warioba’.

IJUMAA WIKIENDA limepiga stori nyinginyingi na Lulu Diva, shuka nayo;

IJUMAA WIKIENDA: Kwanza hongera kwa uzinduzi wa EP (Extended Play) yako wiki iliyopita.

LULU DIVA: Asante.

IJUMAA WIKIENDA: Unazungumziaje mapokeo ya EP yako?

LULU DIVA: Ninamshukuru Mwenyezi Mungu, mashabiki wameipokea vizuri. Mungu awabariki sana.

IJUMAA WIKIENDA: Tumeona kwenye EP yako umewashirikisha mastaa wengi Afrika Mashariki, mipango yako ikoje kufanya kazi na wasanii kutoka nchi nyingine kama akina Tiwa Savage (Nigeria) au hata Beyonce (Marekani)?

LULU DIVA: Mipango ipo, cha muhimu tuombeane maana kila kitu kina hatua na huu ni mwanzo tu, ila huko mbeleni nitafanya vitu vikubwa zaidi.

IJUMAA WIKIENDA: Naogopa ni ngoma ambayo inafanya vizuri, kwa nini uliamua kumchagua Mr Blue na siyo staa mwingine?

LULU DIVA: Hata ukisikiliza ngoma kwa mara ya kwanza, utapata jibu kwa nini nimemchagua Mr Blue. Kwa sababu ni mkongwe na bado anafanya vizuri na mimi napenda kufanya kazi na wasanii wakongwe kwa sababu kunakuwa na ladha fulani ndani yake.

IJUMAA WIKIENDA: Kwenye EP yako tunaona umeshirikiana na mastaa wa kiume tu, kwa nini hakuna msanii wa kike?

LULU DIVA: Ni kwa sababu hii si album, ni EP; yaani ni mjumuiko wa ngoma chache zinazotambulisha album. Kwa kufanya na wanaume tu, nilikuwa natengeneza ladha ya tofauti. Mipango ya kufanya kazi na wanawake wenzangu katika projekti itakayofuata ipo, hivyo mashabiki watajionea vitu vizuri.

IJUMAA WIKIENDA: Katika orodha ya wasanii wa kike wanaofanya vizuri kwenye soko la Bongo Fleva, wewe ni mmoja wapo. Je, nini siri ya mafanikio?

LULU DIVA: Ni kumtanguliza Mwenyezi Mungu. Kufanya kazi kwa bidii kinoma. Pia kuangalia malengo na ndoto zinasemaje. Ndoto yangu ni siku moja kuwa mwanamuziki wa kimataifa, pia kuna kujiamini na kutokukata tamaa.

IJUMAA WIKIENDA: Kuna kipindi wewe na TID mlikuwa kwenye makopakopa na kupostiana kwa sana mitandaoni, lakini baadaye ziliibuka tetesi kuwa mna bifu. Je, uhusiano wako na TID kwa sasa ukoje?

LULU DIVA: Mimi na TID tuko sawa na hatuna bifu, tuko poa kabisa.

IJUMAA WIKIENDA: Unaonekana kuwa karibu na Wasafi Classic Baby (WCB), je, kuna mipango ya wewe kutua kwenye lebo hiyo maana wana uhaba wa wasanii wa kike?

LULU DIVA: Napenda kuwa hivi nilivyo na sina maisha ya utimu hasa kwenye muziki wangu. Wasanii wote ni wangu. Kuwa karibu na mtu au lebo fulani si kwamba mimi ni wa huko, hapana ni uhusiano wa kimuziki tu.

IJUMAA WIKIENDA: Unauzungumziaje urafiki wako na Wema Sepetu?

LULU DIVA: Sina mipaka ya kuwa karibu na watu. Kila mtu ni rafiki yangu.

IJUMAA WIKIENDA: Je, kwa sasa upo kwenye uhusiano wa kimapenzi?

LULU DIVA: Hapana, siko kwenye uhusiano wa kimapenzi.

IJUMAA WIKIENDA: Je, kama utampata, umeshafikiria kufunga ndoa?

LULU DIVA: Ndiyo, kwa sababu kila mwanamke anatamani kuwa kwenye ndoa. Hata mimi natamani sana ndoa ila tatizo ni kwamba kupata mwanaume wa kufunga naye ndoa ndiyo ishu maana sisi wasanii tunaonekana kama watu ambao hatueleweki, wahuni au tuna mambo mengi, kumbe ni kazi tu zinafanya tunafikiriwa hivyo.

IJUMAA WIKIENDA: Siku hizi mastaa wengi wa kike wanapenda kuwa na watoto hata kabla ya ndoa. Je, kwa upande wako vipi?

LULU DIVA: Hivi kuna mwanamke ambaye hatamani mtoto? Basi huyo hatakuwa sawa maana ndoto ya kila mwanamke ni kuwa na mtoto, hata mimi natamani kuzaa.

IJUMAA WIKIENDA: Unawaambia nini mashabiki wako?

LULU DIVA: Waendelee kunisapoti, sitawaangusha!

MAKALA: HAPPYNESS MASUNGA

Leave A Reply