Makambo, Tshishimbi Kurudi na Ubingwa Yanga
NYOTA wa Yanga raia wa DR Congo, Heritier Makambo na Papy Kabamba Tshishimbi, Januari 14 watatua jijini Dar es Salaam, wakiwa na mipango rasmi ya kuisaidia timu hiyo kuibuka na ubingwa wa Ligi Kuu Bara kufuatia mapumziko ya zaidi ya wiki mbili waliyopewa na uongozi wao.
Mpaka sasa Makambo anaongoza chati ya ufungaji kwenye msimamo wa ligi akiwa na jumla ya mabao 11 yanayoifanya timu hiyo pia kuwa kileleni mwa ligi hiyo baada ya kujikusanyia pointi 50.
Yanga hivi karibuni walisimama kucheza mechi zao za ligi na kwenda visiwani Zanzibar kushiriki Kombe la Mapinduzi ambalo hata hivyo juzi walipoteza matumaini ya kuendelea baada ya kufungwa na Malindi 2-1.
Akizungumza na Championi Jumatano, Ofisa habari wa timu hiyo, Dismas Ten alisema; “Hatukuwekeza nguvu kubwa sana kwenye michuano ya Mapinduzi Cup na ndiyo maana utaona vijana walioenda wengi ni kikosi cha pili, hivyo nia yetu na mipango yetu ipo kwenye ligi kuu, baada tu ya kurejea kwao watajumuika na wenzao kwa ajili ya mazoezi ili kufanikisha malengo yetu ya baadaye.”
“Makambo na Tshishimbi wataingia Januari 14 wakitokea Congo ambako walienda kwa mapumziko na kutatua mambo yao ya kifamilia, hivyo tuna imani kuwa mapumziko yao yataleta chachu kubwa katika michezo ijayo maana kila mmoja atakuwa na utimamu mzuri wa mwili ili kufanikisha wazo letu la kutwaa ubingwa,” alisema Dismas.
Stori: Musa Mateja, Championi
Comments are closed.