Mgombea Mwenza wa Urais kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM), Samia Suluhu Hassan ameendelea na ziara ya kuomba kura kupitia Chama Cha Mapinduzi mapema leo katika viwanja vya Mji Mwema, Kigamboni jijini Dar.
Akizungumza wakati wa mkutano huo Mh.Suluhu amesema kuwa miradi yote ambayo Chama Cha Mapinduzi iliyoahidi imetekelezwa na bado inaendelea nayo.
“Tumetekeleza miradi mingi ya Kigamboni na ninawaomba tarehe 28 Tukamilishe kazi iliyokusudiwa kwa kuwa miradi mingi imetekelezwa katika Serikali ya awamu ya tano na nyie ni mashuhuda wa maendeleo yaliyofanyika na ilani imetekelezwa kwa kufanya yote tuliyoyahidi sehemu nyingine yamekamilika na sehemu nyingine yanaendelea.
“Tumeweza kutumia mamilioni ya fedha kwa ajili ya watoto wa shule za msingi na Sekondari kwenye elimu bure na ujenzi wa matundu ya vyoo kwa ajili ya watoto,tumeongeza fedha kwa watoto wetu wa elimu ya juu na miundo mbinu itaendelea kukarabatiwa. Tunakwenda kuimarisha elimu ya watu wazima ili waweze kujua kusoma na kuandika.
“Tumejenga Barabara na madaraja na tutendelea kuimarisha na kujenga barabara za juu 8 ikiwemo barabara za magari yaendayo kasi, kwenye usafiri wa Reli na Ndege pia ujenzi wa Barabara za juu katika maeneo ya Uhasibu, Moroco, Mwenge, Kamata.
“Changamoto ya maji tutaimaliza kwa kuwa tumeshaikabidhi Dawasa baada ya miaka miwili hakutakuwa na changamoto hiyo tena.
Ninawaombee kura Madiwani,pamoja na Mbunge kura ziwe nyingi ili tuweze kusukuma gurudumu la maendeleo,” amesema.
Naye mgombea ubunge kupitia Chama Cha Mapinduzi Dkt. Faustine Ndungulile amesema kuwa miradi yote imetekelezwa kwa mujibu wa Ilani ya Chama.
“Tunatarajia kutakuwa na soko kubwa katika wilaya yetu ambayo itasaidia wananchi waweze kupata bidhaa hapo na kujipatia kipato.
“Kauli mbiu ni Ndungulile mitano tena kwa kuwa mimi nimesimamia nitawalipa maendeleo mafanikio ya utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi ndio maana miradi yote ambayo tuliihaidi tumeitekeleza ikiwemo ujenzi wa Hospitali,vituo vya Afya,” amesema.