MKUU wa Mkoa wa Dar es salaam, Paul Makonda, ametoa taarifa ya kampeni ya usafi iliyoanza takribani mwezi mmoja uliopita kwenye kikao kilichohusisha wadau ya afya na mazingira huku akilaani tena kitendo kilichofanywa na baadhi ya mgambo kupiga raia.
Akizungumza leo jijini Dar es Salaam katika kikao kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Anatoglo, Makonda amesema kuwa tangu kuanza kwa kampeni hiyo zaidi ya watu elfu 10,000 wamekamatwa na watu 4443 waliachiwa huru huku 376 walipata dhamana na takribani watu 6577 walilipa faini iliyofikia zaidi ya shilingi milioni 346 ambapo nusu ya fedha hizo ilikuwa ni malipo kwa mgambo wanaosimamia usafi na hadi sasa watu 6 bado wapo mahakamani.
Makonda amesema kuwa yeye na viongozi wengine wa mkoa wake wamelaani kitendo cha mgambo hao kumpiga raia katika eneo la Bunju na wamefatilia na hadi sasa watuhumiwa wapo katika gereza la Segerea na amewataka mgambo kufanya kazi kwa kufuata sheria.
Aidha amewashukuru wadau na wananchi hasa wale wanaofanya usafi bila shuruti na kuwataka Wakandarasi kufanya kazi kulingana na mikataba yao na kwa kampuni zilizodanganya katika mikataba yao wajiandae kulipa gharama hizo kwa serikali.
Aidha Makonda amewataka wakazi wa jiji la Dar es salaam kushiriki katika shughuli mbalimbali za usafi huku akiwataka wafanyabiashara na wenye viwanda kuweka mazingira yao katika hali ya usafi.
Kwa upande wake Katibu Tawala wa Mkoa huo, Abubakar Kunenge amesema kuwa suala la usafi ni la wajibu wa kila mmoja kuhakikisha jiji linakuwa safi huku akiwaomba wadau wa afya na mazingira kuhamasisha katika suala zima la mazingira.
Mkutano huo umeshirikisha wadau na taasisi mbalimbali za mazingira ambao kwa amoja wamejadili namna ya kuweka jiji katika hali bora zaidi.
Comments are closed.