The House of Favourite Newspapers

Makosa wafanyayo wapenzi wawapo chumbani-2

0

Blog-pic-couple-cuddling-4441652 (1)Heri ya Mwaka Mpya! Mimi na wewe tunapaswa kumshukuru Mungu kwa kutuvusha salama kutoka mwaka 2015 mpaka leo hii tunapouanza mwaka mwingine wa 2016. Ni wiki nyingine tunapokutana tena katika ukurasa wetu huu mzuri. Wiki iliyopita tulijadiliana kwa kina kuhusu makosa wanayoyafanya wanandoa wengi wawapo vyumbani na wenzi wao.Leo tunaendelea kuanzia pale tulipoishia wiki iliyopita.

2. KUWA BIZE NA SIMU AU TV MUDA WA KULALA
Utandawazi umekuja na mambo mengi, simu zenye intaneti (smartphones) zimegeuka na kuwa kero kubwa kwa wanandoa au wapenzi wanaoishi pamoja. Unakuta mume au mke, muda wa kulala ukifika, anapanda kitandani na simu yake.

Badala ya kuwa pamoja na mwenzi wako kwa mazungumzo ya hapa na pale, kubadilishana mawazo na kubembelezana wakati mkitafuta usingizi, unakuta mtu yuko bize na simu, mara aingie kwenye magroup ya WhatsApp, Instagram, Facebook au Twitter. Hakuna tabia inayoweza kukuweka mbali kihisia na mwenzi wako kama hii.

Wengine unakuta anapanda kitandani akiwa na laptop au anawasha TV ya chumbani na kuanza kuangalia movie au tamthiliya. Matokeo yake, unasababisha mwenzi wako akose usingizi mzuri na hata akipata, analala akijisikia vibaya kwa sababu anaona uwepo wake hauna maana yoyote kwa mwenzi wake.

3. KUWA ‘BUBU’ MKIWA CHUMBANI
Wapo baadhi ya wanandoa au wapenzi ambao wanapoingia chumbani, kila mmoja anajifanya kuchoka sana kiasi kwamba huyu anajitupa kitandani na kugeukia kule, huyu naye anageukia upande mwingine na muda mfupi baadaye, unasikia kila mmoja anakoroma.

Hakuna jambo linalonogesha mapenzi kama mazungumzo ya chumbani wanayoyafanya wanandoa au wapenzi kabla ya kupitiwa na usingizi, Wazungu wanaita ‘Pillow talks’.

Si vibaya kuzungumza na mwenzi wako kwa sauti ya kubembeleza, ukamuuliza jinsi siku yake ilivyokuwa, ukampa pole kwa majukumu ya kutwa nzima. Mazungumzo ya namna hii huwaweka karibu zaidi wanandoa kimwili na kihisia.

4. KUKOSA KAULI NZURI
Nimewahi kupata malalamiko kutoka kwa mdau mmoja ambaye alisema mwenzi wake amekuwa na tabia ya kumjibu kwa mkato, kumtolea lugha chafu au kumfokea hata katika muda ambao hakuna alichomkosea.

Matokeo yake, ule uchangamfu kati ya mtu na mwenzi wake unapungua na kuendelea kufifia kadiri siku zinavyozidi kusonga mbele, baadaye unaanza kumuona mwenzio kuwa mtu wa kawaida, hisia za mapenzi zinapotea kabisa. Hata kama umejizoesha muda wote kuwa ‘serious’, jitahidi kufurahi na mwenzi wako japo kwa dakika chache kabla ya kulala, hii itaongeza ukaribu kati yenu.

5. KUKOSA USAFI WA MWILI
Baadhi ya wanandoa, wakishaanza kuishi maisha ya wawili, hujisahau hata katika yale mambo ya msingi yanayoweza kuboresha mapenzi. Unakuta mtu anapanda kitandani akiwa mchafu, mwili unatoa harufu za ajabu, kikwapa kinanuka, harufu kali inatoka mdomoni na vitu vya namna hiyo.

Unafikiri mwenzi wako atavutiwa kukumbatiana na wewe au kuzungumza kimahaba? Utakuwa kero kwake na atatamani kila mmoja angekuwa na kitanda chake. Kama wewe ni mwanamke, hakikisha ukishamaliza majukumu yako ya kutwa nzima, unatenga muda wa kuoga vizuri na kujipamba, kama una manukato huo ndiyo muda wake.

Itaendelea wiki ijayo.

Leave A Reply