The House of Favourite Newspapers

Mastaa 14 wampasua kichwa Gomes Simba

0

 

KOCHA mkuu wa Simba, Didier Gomes amesema kuwa kukosekana kwa wachezaji wake 14 ndani ya kikosi hiko kinafanya mipango mingi ya timu hiyo kukwama katika maandalizi ya timu hiyo kuelekea katika mchezo wa kimataifa dhidi ya Jwaneng Galaxy ya nchini Botswana.

Wachezaji hao wa Simba ni wale ambao wameitwa na timu zao za taifa kwa ajili ya michezo ya kufuzu Kombe la Dunia litakalofanyika nchini Qatar 2022.

Mastaa hao ni pamoja na Aishi Manula, Mohamed Hussein, Mzamiru Yassin, John Bocco, Erasto Nyoni, Israel Mwenda, Kennedy Juma na Kibu Denis wote wakiitwa timu ya taifa ya Tanzania. Wengine ni Joash Onyango (Kenya), Taddeo Lwanga (Uganda), Rally Bwalya (Zambia), Peter Banda na Duncan Nyoni (Malawi) na Meddie Kagere aliyeitwa Rwanda.

Akizungumza na Championi Jumamosi, Gomes alisema kuwa kukosekana kwa wachezaji hao kunapunguza kitu haswa katika mipango ya mbinu mbalimbali ndani ya kikosi hiko katika kuelekea mchezo huo na Jwaneng Galaxy jambo ambalo haliepukiki kutokana na ratiba za kimataifa kuwaruhusu mastaa hao kushiriki michezo ya kimataifa.

“Huwezi kuwazuia wachezaji kwenda kushiriki michuano ya kimataifa kwa kuwa ipo katika ratiba duniani kote katika ligi mbalimbali. Lakini kuwakosa wachezaji 14 ndani ya timu tukiwa katika maandalizi ya mchezo wetu muhimu dhidi ya Jwaneng kuna kitu kinapungua haswa katika masuala ya mbinu kuelekea katika mchezo huo.

“Lakini bado tunayo nafasi ya kufanya vizuri kwa kuwa tuna kikosi imara cha kupambana kwa ajili ya kupata matokeo mazuri, tunaelekea ugenini na tutafanya kila uwezekano kupata matokeo mazuri, malengo yetu siku zote ni kufanya vizuri,” alisema kocha huyo.

 

 

 

MARCO MZUMBE NA HAWA ABOUBAKHARI,Dar

Leave A Reply