GEORGE Majaba, mshindi wa Bahati Nasibu ya Shinda Nyumba Awamu ya Pili, Jumanne Oktoba 31, 2017 amewasili jijini Dar es Salaam tayari kwa zoezi la kukabidhiwa nyumba yake aliyojishindia baada ya droo kubwa iliyochezwa Septemba 27, mwaka huu.
Katika mapokezi hayo yaliyopambwa kwa pikipiki, gari la wazi, muziki na madansa, Majaba aliwasili katika ofisi za Global Group, zilizopo Sinza Mori mishale ya saa tisa na ushee hivi na kupokelewa na wafanyakazi ambao walimpigia makofi ya shangwe na baadaye kumwimbia nyimbo ya kumsifu kwa ushindi.
Mara baada ya kukaribishwa katika ukumbi wa mikutano wa kampuni, Meneja Mkuu wa Global Group, Abdallah Mrisho alimkaribisha Mkurugenzi Mtendaji Eric Shigongo ambaye baada ya kumkaribisha Majaba na mkewe, Neema, alimshukuru Mungu kwa ndoto zake kutimia.
“Siku zote nimekuwa nikiomba Mungu kuwa zawadi hizi tunazotoa, zifike kwa watu wenye uhitaji, tunapotoa zawadi ya nyumba, niliomba iende kwa mtu mwenye uhitaji wa nyumba kweli, kwa sababu tunataka kubadilisha maisha ya watu.
“Niwe mkweli, kama zawadi hii angeipata mtu ambaye tayari ana nyumba tano, nisingefurahi kabisa, lakini kwa mujibu wa makala zako nilizokuwa nasoma, wewe unaishi kwenye nyumba ya kupanga, kwa maana hiyo siku zote ulikuwa ukiomba upate nyumba na leo Mungu amekubariki.
“Wewe utakuwa balozi mzuri wa Global Group kwa sababu watu wengi wamekuwa wakisema kuna ujanjaujanja katika zawadi, nina uhakika kabla ya leo hakukuwa na mtu yeyote unayemjua hapa, lakini wewe umejikuta ukipata nyumba. Tunakukaribisha sana na asante Mungu kwa ndoto zetu kutimia,” alisema.
Baada ya kukaribishwa na kuzungumza machache na wafanyakazi na baadaye kutembezwa katika vitengo mbalimbali vya Global Group, Majaba na familia yake waliondoka kuelekea Bunju B, ambako ndipo ilipo nyumba yake ya kisasa na hivyo kuwa miongoni mwa wamiliki halali wa nyumba za kisasa katika Jiji la Dar es Salaam.
Na Mwandishi Wetu.