The House of Favourite Newspapers

Mtemvu alivyotoa siri za Nyerere- 10

0

mtemvu na nyerereTunaendelea kusimulia yaliyojiri baada ya Zuberi Mtemvu kukosana kisiasa na Mwalimu Julius Nyerere:

Baada ya uhuru, Mwalimu Julius Nyerere aliendelea kushikamana na baadhi ya watu waliokuwa wakiheshimika katika jamii huku Zuberi Mtemvu akiwa adui yake rasmi kisiasa.

Mmoja wa wazee waliompokea Nyerere jijini Dar ni Abdulwahid Sykes. Kabla hajafariki dunia Abdulwahid alifanya mazungumzo na Nyerere.

Mazungumzo hayo baina ya Abdulwahid na Nyerere yalifanyika katika miezi ya mwisho ya mwaka 1968 huku watu mashuhuri wakisombwa na kutupwa gerezani kwa sababu zilizotajwa kuwa za kiusalama.

Abdulwahid na Nyerere walikuwa wametoka mbali. Watu hawa walikuwa marafiki wa zamani. Huenda kama isingelikuwa kwa msaada wa Abdulwahid historia ya Tanu na ya Nyerere zingechukua mkondo tofauti.

Mazungumzo haya yalikuwa muhimu kwa Abdulwahid kwa sababu kwa kiasi fulani alihisi anahusika na yale yaliyokuwa yakiwasibu watu hao maarufu wa Dar es Salaam.

Taarifa za kukamatwa watu mbalimbali baada ya uhuru na kuwekwa kizuizini zilikuwa zikimfikia karibu kila siku Abdulwahid na hakuweza kujifanya kuwa haathiriki na vitendo vile.

Baadhi ya watu ambao Nyerere alikuwa anawatupa gerezani walikuwa watu ambao yeye Abdulwahid walimuunga mkono wakati anaanza siasa na watu ambao aliwashawishi wamkubali Nyerere wakati wa kuundwa Tanu.

Abdulwahid alimwambia Nyerere huenda yeye akawa hana hisia wala uhusiano wowote na watu ambao yeye anatia sahihi wakamatwe na kutupwa gerezani. Lakini kwake yeye hao ni jamaa zake anaokutananao ama msikitini au mitaani. Yeye kama mtu anayeishi miongoni mwao na zile familia zao alikuwa anaelewa majonzi yao.

Abdulwahid alimwambia Nyerere kwamba watu wale wanajua kuwa yeye, Abdulwahid ndiye aliyemsaidia Nyerere wakati akiwa mgeni mjini Dar es Salaam, watu wakamjua na kumkubali hivyo kuweza kufika hapo alipofika.

Abdulwahid alimwambia Nyerere kuwa ndugu na jamaa aliowafungwa wanamjia wakimbembeleza amsihi Nyerere awatoe ndugu zao jela.

Itaendelea wiki ijayo.

Leave A Reply