Shambulio la Kigaidi Laua Wanne Jerusalem
WATU wanne wameuawa mchana huu jijini Jerusalem, Israel, katika shambulio la kigaidi baada ya mtu mmoja kulielekeza lori alilokuwa analiendesha katika kundi la kuwaua watu na kujeruhi wengine wasiopungua 15. Waliouawa ni wanawake watatu na mwanamme moja ambapo, taarifa za polisi na mashuhuda zilisema, mtu huyo baada ya kuliingiza gari hilo katika kundi la watu, alilirudisha nyuma na kuwakanyaga watu hao waliokuwa wameanguka.
Taarifa hizo zilisema pia kwamba mshambuliaji huyo alipigwa risasi na wanajeshi waliokuwa karibu lakini haikufahamika kama alikufa.
Mitandao imeonyesha lori hilo likiwa na matundu ya risasi kwenye kioo chake cha mbele ambapo ripoti za radio na televisheni zilisema mshambuliaji alikuwa Mpalestina.
Waisrael 35 wameshauawa katika wimbi la mashambulio ya visu, bunduki na kutumia magari yanayofanywa na Wapalestina au Waarabu wa Israel tangu Oktoba 2015. Vilevile, Israel imesema Wapalestina 200, wengi wao wakiwa washambuliaji, wameuawa katika kipindi hicho.
Israel imekuwa ikisema uchokozi huo ndiyo umeongeza mashambuliano kati ya pande hizo, ambapo uongozi wa Wapalestina umelaumu Israel kuendelea kukalia kwa nguvu maeneo yao.
Salum Milongo/GPL
.
Comments are closed.