The House of Favourite Newspapers

Mwakinyo Namba 1 Tanzania, Apanda Nafasi Ubora Duniani

0

MWAKINYO aliyewahi kuwa namba moja Afrika na wa 14 duniani baada ya kumchapa kwa TKO, Samm Eggington wa Uingereza aliyekuwa bondia namba nane wa dunia kwenye uzani wa Super Welter mwaka 2018, mwanzoni mwa mwaka huu aliporomoka hadi nafasi ya 86 duniani.

 

Amepanda kwa nafasi 14 katika viwango vya ngumi duniani, huku akitajwa kuwa bondia namba moja nchini. Kwa mujibu wa viwango vipya ya mtandao wa ngumi za kulipwa wa dunia (Boxrec), Mwakinyo sasa ni bondia wa 72 duniani kutoka nafasi ya 86 aliyokuwepo awali kwenye uzani wa super welter anaopigania.

 

Katika ubora wa mabondia wa kila uzani (Pound for Pound), Mwakinyo ameingia kwenye ‘top 50’ ya Afrika inayoongozwa na Junior Makabu na Richard Commey wanaopigania uzani wa Cruiser raia wa DR Congo na Kevin Lerena anayepigania uzani wa light raia wa Afrika Kusini amehitimisha tatu bora.

 

Nchini Mwakinyo amepanda na kuwa bondia namba moja kwenye pound for pound huku Ibrahim Class bondia wa uzani wa super feather akishuka hadi nafasi ya pili.

 

Abdallah Pazi (Dullah Mbabe) anayepigania uzani wa super middle amehitimisha tatu bora katika pound for pound ya Tanzania huku kidunia, Saul Alvarez wa Mexico anayepigania uzani wa middle ndiye namba moja.

 

Bondia wa uzani wa juu, Tyson Furry ndiye namba mbili na Errol Spence Jr amehitimisha tatu bora ya dunia huku mabondia kama Manny Pacquiao na Anthony Joshua wakiingia kwenye kumi bora ‘top ten’ ya dunia.

 

Nchini Tanzania mabondia wengine walioingia kwenye kumi bora ni Twaha ‘Kiduku’ Kassim, Tony Rashid, Fadhil Majiha, Salim Mtango, Hamis Maya, Muhsin Kizota na Iddi Pialari.

 

Akizungumzia rekodi hiyo, Mwakinyo ambaye amecheza mapamba 19 na kushinda 17 alisema anaamini atapanda zaidi ya hapo na kurudi kwenye rekodi yake ya mwaka mmoja uliopita.

Leave A Reply