The House of Favourite Newspapers

Sasa Waweza Kununua Tiketi za Michezo Kidigitali na Tigo Pesa

0
Kaimu Afisa Mkuu wa Tigo Pesa, Angelica Peter, akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) wakati wa uzinduzi mfumo kwa ajili ya kuwarahisishia mashabiki wa soka kununua tiketi kwa njia ya Tigo Pesa katika michezo mbalimbali itakayochezwa Uwanja wa Uhuru na Mkapa, Dar es Salaam.

KAMPUNI ya simu za mkononi ya Tigo na Kituo cha Taifa cha Kuhifadhi Data Kimtandao (NIDC), zimeungana kwa ajili ya kuwarahisishia mashabiki wa soka kununua tiketi kwa njia ya Tigo Pesa katika michezo mbalimbali itakayochezwa Uwanja wa Uhuru na Mkapa, Dar es Salaam. Mashabiki wa soka wataanza kunufaika na huduma hiyo ya kisasa ili kuhakikisha wanapunguza msongamano wakati wa kukata tiketi kwa ajili ya kwenda kuangalia mechi za soka kwenye viwanja hivyo.

Akizungumza Dar es Salaam, Kaimu  Afisa Mkuu wa Tigo Pesa, Angelica Peter, alisema kuwa wameungana na NIDC kwa ajili ya kuwasaidia mashabiki wa soka kukata tiketi kwa njia ya mtandao.Alisema kuwa mashabiki wa soka kwa sasa watakuwa wamepunguza suala la kutembea na fedha taslimu na badala yake wataanza kutumia huduma ya kukata tiketi kwa njia ya Tigo Pesa.

“Wateja wetu kwa sasa hawatapata tabu tena au kuhangaika kufanya malipo ya tiketi za michezo, kwani kupitia Tigo Pesa wanaweza kufanya malipo ya tiketi kidijitali kupitia kadi maalumu kutoka kwa washirika wetu kituo cha Taifa cha Kuhifadhi Data Kimtandao cha (NIDC).

“Tanzania ni moja ya nchi za kuigwa katika kufanya malipo kidijitali au kielektroniki. Kupitia malipo haya ya N-Card tumeendelea kupeperusha bendera katika nyanja ya malipo ya kidijitali,” alisema

Afisa Uhusiano wa Kituo cha NIDC, Geophrey Mlelwa, alisema kuwa wamefurahia kuungana na Tigo kwa ajili ya kuleta mapinduzi kwenye michezo.

Mkurugenzi wa Michezo Tanzania, Yusuf Singo akizungumzia huduma hiyo jinsi itakavyoleta mapinduzi ya kuondoa kero viwanjani.

 

Alisema kuwa mashabiki wa soka watapata fursa ya kukata tiketi za kuangalia mechi mbalimbali bila tatizo lolote kuanzia sasa.”Hii ni fursa kwa wapenzi wa michezo hasa mpira wa miguu kuweza kununua tiketi kirahisi na kwa haraka bila bughudha yoyote kupitia kadi hii maalum (N-card) ambapo watafanya malipo kupitia Tigo Pesa.” alisema Mlelwa.

Mkurugenzi wa Fedha wa  Yanga, Mfikirwa Hajji, alisema kuwa mashabiki wa Yanga watumie fursa hiyo hasa katika mechi yao dhidi ya Simba itakayochezwa Jumamosi. Alisema mechi hiyo hukusanya mashabiki wengi zaidi na kwamba amewataka kununua tiketi zao mapema kwa ajili ya kuahudia mchezo huo.

“Hii ni fursa ya aina yake na kwamba tunawaomba mashabiki wetu waitumie kila wakati kwa kuanzia katika mechi yetu dhidi ya Simba itakayofanyika Jumamosi,” alisema.

Leave A Reply