KUFUATIA mapigano ya mara kwa mara ya wakulima na wafugaji sambamba na migogoro ya kugombea mipaka, umepatiwa ufumbuji Kijijini Melela Wilaya ya Mvomero mkoani Morogoro baada ya wakulima wa Kijiji hicho kupimiwa mashamba yao na kukabidhiwa hatimiliki kwenye semina maalum iliyoandaliwa na Uongozi wa Kitengo cha Urasimishaji Rasilimali Ardhi Vijijini (MKURABITA).
Katika semina hiyo, kati ya wakulima zaidi ya 300 wa kijiji hicho, ni wananchi 100 pekee ndiyo waliyoelewa vizuri somo hilo na kutimiza vigezo vya kupimiwa mashamba yao na juzi Oktoba 31, 2018 kisha kukabidhia hati miliki za kimila na maofisa ardhi hao.
Akizungumza baada ya semina hiyo, mmoja wa wakulima wa kijiji hicho, mzee Anthony Maloko aliishukuru serikali kuwapelekea semina hiyo ambayo imekuwa chachu ya kuwakwamua na kuondokana na migogoro iliyokuwa ikijitokeza hapo awali.
“Semina kama hizi walikuwa wakifanya vigogo serikalini pamoja na wafanyakazi wao, hata siku moja hapa kijijini hatujawahi kuletewa semina yoyote kama hii, tumeelimishwa jinsi ya kupimaa mashamba yetu.
“Tumepewa hatimiliki ambazo kimsingi utakuwa ni mwarobaini wa ugomvi wa mipaka kati ya wakulima majirani, pia kati ya wakulima na wafugaji. Licha ya uzee wetu, lakini tulifundishwa jinsi ya kutumia fursa za hapa kijijini ilikujikwamua kimaisha,” alisema mzee Maloko.
Aidha, kwa upande wake, Meneja wa MKURABITA, Anthony Temu akizungumza na globalpublishers.co.tz alisema lengo la semina hizo ni kupima mashamba na kuwapa wakulima hati za kimila sambamba na kuwafundisha kulima kilimo cha kisasa kwa lengo la kupata mazao mengi.
Na Dunstan Shekudele, Morogoro.
Comments are closed.