Naibu Waziri Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (MB) ametembelea Chuo Kikuu Mzumbe na kukagua ujenzi wa Mabweni ya Wanafunzi unaoendelea katika eneo la Maekani, Makao Makuu ya Chuo hicho, Morogoro.
Mhe. Naibu Waziri, amepongeza jitihada kubwa zilizofanywa na Uongozi wa Chuo kwa kushirikiana na Serikali katika kutatua kero ya malazi kwa wanafunzi na kusisitiza umuhimu wa kuanza mara moja awamu ya pili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa na mihadhara katika eneo hilo ili kuwarahisishia wanafunzi kutotembea umbali mrefu wakati wa masomo.
“Serikali inategemea mchango mkubwa wa Vyuo Vikuu katika kutimiza malengo; hasa kwenye hili la ukuaji wa uchumi. Pamoja na kwamba tunajivunia uchumi wetu kukua lakini tusibweteke, badala yake tufanye tafiti na kuandaa vyema vijana ambao watakuwa watumishi bora wa Umma wanaoendana na dhana ya sasa ya nidhamu ya kazi. Hivyo, nimefarijika sana kuona maendeleo na hatua kubwa ambayo mmepiga kitaaluma na katika miradi ya maendeleo mnayosimamia” alisema Mhe. Naibu Waziri.
Akimkaribisha Naibu Waziri huyo, ambaye pia alipata fursa ya kuzungumza na Menejimenti ya Chuo Kikuu Mzumbe; Makamu Mkuu wa Chuo, Prof. Lughano Kusiluka amemweleza Mheshimiwa Naibu Waziri kuwa, kwa sasa Chuo Kikuu Mzumbe kinatekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo ya miundombinu katika Kampasi Kuu ya Morogoro, Kampasi ya Mbeya na Kampasi ya Dar es Salaam na kwamba, lengo ni kuendelea kutumia ruzuku inayotolewa na Serikali na vyanzo vya mapato ya ndani kuendeleza ujenzi na kuboresha miundombinu ya Chuo ili kujenga mazingira bora ya utoaji wa Elimu ya Juu.
“Napenda kuipongeza sana Serikali yetu kwa kutambua mchango mkubwa wa Vyuo Vikuu nchini, na kwa upande wa Taaluma, Chuo chetu kitaendelea kuunga mkono jitihada za Serikali ya Awamu ya Tano katika kuendeleza Uchumi wa Viwanda; kwa kuendelea kufanya tafiti, kubuni miradi ya maendeleo na kutoa nguvu kazi itakayowezesha Tanzania kufikia malengo yake” alisema Prof. Kusiluka.
Ameahidi Chuo Kikuu Mzumbe kuendelea kuimarisha uhusiano na kufanya kazi kwa karibu zaidi na Taasisi na Mashirika mbalimbali ya Umma kwa kubadilishana ujuzi na uzoefu, pamoja na kutumia wanataaluma kuboresha utendaji Serikalini, kulinda nidhamu na kuinua kiwango cha elimu inayoendelea kutolewa na Chuo hicho.
Mradi wa Ujenzi wa Mabweni katika Kampasi Kuu ya Chuo Kikuu Mzumbe ambao unafadhiliwa na Serikali,unatekelezwa na SUMA JKT na unategemewa kukamilika ifikapo mwezi Oktoba mwaka huu. Mradi unategemea kugharimu kiasi cha shilingi bilioni 6.5 hadi utakapokamilika. Kukamilika kwa mradi huu kutawezesha wanachuo wengi zaidi katika Kampasi Kuu kukaa kwenye hosteli za Chuo.
Comments are closed.