The House of Favourite Newspapers

Pablo Awapiga Stop Mastaa Simba Kula Chipsi Zege

0

KOCHA Mkuu wa Simba, raia wa Hispania, Pablo Franco, amemtaka kiungo kisiki wa timu hiyo, Mganda, Thadeo Lwanga, kuepuka matumizi ya vyakula vya mafuta mengi kipindi hiki ambapo bado yupo kwenye program maalum.

 

Lwanga yupo nje ya kikosi hicho akiuguza majeraha ya goti lake aliyoyapata takriban miezi miwili iliyopita wakati timu hiyo ikicheza mchezo wa Ligi ya Mabingwa dhidi ya Jwaneng Galaxy FC ya Botswana, uliomalizika kwa Simba kupigwa 3-1, na kuondolewa katika mashindano hayo.

 

Chanzo chetu kimeliambia Championi Ijumaa kwamba, takriban wiki sasa kocha wa Simba, Pablo amemtaka Lwanga kujiepusha na utumiaji wa vyakula vyenye mafuta mengi zikiwemo chipsi mayai, ili aweze kupona mapema, maana anahitaji huduma yake kwani tangu aungane na Simba hajawahi kumuona akicheza.

 

“Kadiri mambo yanavyozidi kuwa magumu kikosini kocha naye ameendelea kuwasisitiza wachezaji kujiepusha na vyakula vyenye mafuta mengi kama vile chipsi, nyama nyekundu na hata utumiaji wa vinywaji vyenye sukari nyingi, ili waweze kupunguza hali ya kupata majeraha.

 

“Tangu kocha Pablo atue kikosini amekuwa na kawaida ya kuchunguza vyakula vya wachezaji na kwamba amekuwa akikemea vikali anapoona hali ya wachezaji kupenda vyakula vya aina hiyo, hasa kwa wenye majeraha kama ilivyo kwa Lwanga ambaye kwa sasa yupo kwenye program maalum,” kilisema chanzo hicho.

 

Championi limethibitisha kwa Afisa Habari wa Simba, Ahamed Ally, ambaye amesema: “Kweli kocha amekuwa akifuatilia hali za wachezaji wote, ila kwa sasa Lwanga amepewa takriban wiki tatu awe amekamilisha programu na Mungu akimjalia hadi mwisho wa mwezi huu atakuwa amerejea.”

MUSA MATEJA, Dar es Salaam

Leave A Reply