The House of Favourite Newspapers

Profesa Msomi Zaidi Duniani Mwenye Shahada 145

0
Prof. Dhamira ya V.N. Parthiban.

KAMA unafikiri kupata shahada (digrii) ni kazi ngumu, tangu sasa fahamu kwamba Profesa V.N. Parthiban anayefundisha jijini Chennai, India, ana shahada 145 alizozipata katika kipindi cha miaka 30!

Si hivyo tu, jamaa huyo bado ana mipango ya kujiendeleza kielimu. Safari ya Parthiban ilianza wakati anasomea shahada yake ya kwanza ambapo alikuwa anachanganya mambo katika masomo yake ya majaribio, na hivyo kujikuta akifanya vibaya katika mitihani na miradi muhimu chuoni.

Baada ya kuhitimu, alipata kazi katika Idara ya Mahakama, lakini dhamira ya kujiendeleza ilibakia palepale. Akiwa amevutiwa na masomo ya fani mbalimbali za masomo chuoni, Parthiban aliamua kurejea chuoni ambako alipata shahada ya pili, ya tatu na kisha akaongeza zingine 142.

Katika mahojiano yake na jarida la Sunday Indian, msomi huyo anasema: “Nilianza kutuma maombi katika vyuo ambavyo havikuhitaji cheti cha uhamisho katika usajili ili niweze kusoma kozi mbalimbali wakati mmoja. Katika miaka thelathini iliyopita nimekuwa najiandaa mfululizo kufanya mitihani na kutuma maombi ya kozi za shahada na stashahada (diploma).”

Prof. V.N. Parthiban akikabidhiwa tuzo.

Orodha ya mafanikio ya Parthiban inajumuisha shahada za uzamili (master) katika masomo yafuatayo: shahada tatu za sayansi, shahada nane za sheria, shahada nane za biashara, shahada tisa za utawala katika biashara, shahada 10 za sanaa, na shahada 12 za utafiti mbalimbali. Alipoulizwa iwapo kuna somo ambalo hapendi kulisomea, Parthiban alijibu moja kwa moja kwamba ni “hisabati”.

Kwa bahati mbaya, kumekuweko na athari kadhaa za kusoma kwa muda mrefu kwa upande wa Parthiban. Kusoma sana kumeathiri kumbukumbu za Parthiban kwani hivi sasa ana matatizo ya kukumbuka sura za watu na njia ambazo amezipita kwa muda mrefu.

Hata hivyo, matatizo hayo hayajamkatisha tamaa mtu huyo msomi mwenye umri wa miaka 56 bado anafanya uhadhiri katika masomo mbalimbali katika vyuo. Mbali na shughuli zake za kisomi, Parthiban ana familia – mke na watoto wawili — ambapo nao wamejikita katika masomo kama alivyofanya.

Mke wake hadi sasa ana shahada tisa, hivyo anahitaji zingine 136 ili amfikie mumewe. Dhamira ya V.N. Parthiban inawakumbusha walimwengu jina la Luciano Baietti, ambaye anashikilia rekodi ya dunia ya kuwa mtu mwenye idadi kubwa zaidi ya shahada za vyuo vikuu.

Leave A Reply