Queen Masanja Na Kampuni Ya Fixchap Watoa Msaada Wa Vitakasa Maji Kwa Watoto Wanaouguzwa Saratani
Dar es Salaam 11 Novemba 2023: Mrembo Queen Masanja ambaye ni balozi wa Kampuni ya kutakasa maji ya Fixchap, leo wamewakumbuka watoto wanaouguzwa saratani kwenye jengo la Tumaini la Maisha lililopo Hospitali ya Taifa ya Muhimbili jijini Dar es Salaam kwa kuwapa vitakasa maji aina ya Ecofilter.
Akizungumza kwenye tukio la kukabidhi msaada huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Fixchap Tanzania, Prince Tillya ambao ni wasambazaji wa bidhaa hiyo amesema kabla ya kuanza kuisambaza kwa wateja wanaohitaji kwa matumizi yao binafsi wameonelea waanze kufanya matendo ya huruma kwa jamii kwa kugawa vitakasa maji hivyo kwa watoto hao walioonekana kuhitaji maji safi na salama kwa kiasi kikubwa.
Naye balozi wa kampuni hiyo, Queen Masanja amesema alikubali kuwa balozi wa kampuni hiyo baada ya kuona umuhimu wa kifaa hicho cha kutakasa maji kinavyokwenda kuokoa afya ya jamii kwa kuepukana na kunywa maji yasiyo salama.
Queen Masanja amewaomba Wasamaria Wema wengine kuwakumbuka watoto hao wanaohitaji misaada mbalimbali katika kupambania afya zao ili waweze kupona na kutimiza ndoto zao.
Akihitimisha tukio hilo, Meneja Mawasiliano wa Taasisi ya Tumani la Maisha, Jenny Chegeni amesema taasisi hiyo ambayo jukumu lao kubwa ni kutunza na kutibu watoto wenye saratani hapa nchini. Jenny aliendelea kusema;
“Leo tumepokea msaada wa vitakasa maji vya ecofilter kutoka Kampuni ya Fixchap, huu ni msaada mkubwa sana kwetu kwasababu tumekuwa na changamoto kubwa sana ya kupata maji safi na salama ya kunywa lakini sasa tatizo hilo limeisha.
“Hivyo tunaishukuru sana kampuni hii kwa kutukumbuka na tunawaomba Wasamaria wema wengine na kukumbuka matendo ya huruma kama haya na kuja kuwasaidia watoto hawa kwenye kituo hiki cha Tumaini la Maisha”.
Kifaa hicho kinauwezo wa kutakasa maji ya aina yeyote na kuwa safi na salama hivyo kuwaepusha wananchi na maradhi mbalimbali yanayosababishwa na maji yasiyo salama.