Shilole ‘Alia’ na Kipigo Kutoka kwa Mumewe
MSANII wa muziki wa Bongo Fleva na mjasiriamali, Zuwena Mohamed, maarufu kama Shilole, ameamua kuweka wazi matatizo ya ndoa yake kupitia ukurasa wake wa instagram. Shilole ambaye ni mke wa ndoa wa Ashrafu Sadiki maarufu kama ‘Uchebe’ ameeleza siri ya ‘Manyanyaso na Vipigo’ aliyokaa nayo kwa muda mrefu ndani ya ndoa yake.
Kupitia ukurasa wake wa instagram, Shilole amewaomba radhi Watanzania, hususan wanawake wenziye kwa kuificha siri hiyo kwa muda mrefu na kuwaaminisha kuwa ndoa yake haikuwa na tatizo lolote, wakati uhalisia wa mambo ni tofauti kabisa.
Katika post yake hiyo iliyowagusa sana Watanzania, Shilole ameambatanisha picha kadhaa zikimuonyesha akiwa na majeraha sehemu za usoni na kichwani, ambazo anadai ni baadhi ya picha za matukio tofauti ya unyanyasaji aliyowahi kuyapitia kutoka kwa Uchebe.
Mwisho wa post hiyo ameeleza kuwa amechoka kuvumilia mateso, na ameamua kuachana na ndoa hiyo na asitambulike tena kama mke wa Ashrafu ‘Uchebe’ na kuwaasa wanawake wenzie kutoficha unyanyasaji wanaokutana nao katika ndao zao.