The House of Favourite Newspapers

Simba SC Wapangua Fitina Botswana

0

JESHI la watu watatu wa Simba waliotangulia nchini Botswana kuandaa mazingira ya timu hiyo kufikia limeanza na kazi ya kupangua fitina za wapinzani wao hao, ambapo wamejipanga kuipeleka timu hiyo kwenye hoteli ya kificho ili kuzuia uwezekano wa kufanyiwa fitina.

 

Simba Jumapili ijayo watakuwa ugenini nchini Botswana kwa ajili ya mchezo wao wa kwanza wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Jwaneng Galaxy, ambapo mchezo huo wa hatua ya kwanza unatarajiwa kupigwa kwenye Uwanja wa Taifa wa Botswana.

 

Tayari Simba imetanguliza timu ya watu watatu wakiongoza na mratibu wa klabu hiyo Abbas Ally na mpishi wao Sam kwa ajili ya kuandaa mazingira kabla ya timu hiyo kutua.

 

Chanzo chetu cha ndani ambacho ni sehemu ya timu hiyo ya watu watatu waliotangulizwa na Simba kimeliambia Championi Jumatano: “Tunashukuru tumefika salama hapa Botswana na maandalizi yote ya kupokea kikosi yanaenda vizuri, hali ya hewa haina tofauti sana na ile ya huko nyumbani japo huku kuna baridi kiasi, lakini tunaamini haiwezi kuwa kikwazo kwa wachezaji wetu.

 

“Wenyeji wetu wanauchukulia mchezo huu kama fainali kwao hivyo wamepanga hujuma nyingi dhidi yetu, lakini kwa kuwa tayari tumeshtukia mchezo tumejipanga kuchukua tahadhari zote ikiwemo hoteli tutakayofikia kuwa na viwanja vya mazoezi, ili kupunguza safari zisizokuwa na lazima lakini pia kuhakikisha wachezaji wetu hawatoki hadharani mara kwa mara na hata watakapolazimika kufanya hivyo basi itakuwa chini ya ulinzi.”

 

Akizungumza na gazeti hili kocha mkuu wa Simba Didier Gomes kuhusu maandalizi ya kikosi chake alisema: “Tunajua wazi kuwa mchezo wetu wa ugenini utakuwa kama vita kutokana na ubora wa wapinzani wetu, lakini tuko tayari kupambana na kupata matokeo bora.”

Musa Mateja na Joel Thomas, Dar es Salaam

Leave A Reply