Simba: Yanga Inatupa Ubingwa baada ya kupoteza dhidi ya Ihefu kwa mabao 2-1
UONGOZI wa Simba, umesema kwamba, kupoteza kwa Yanga katika mchezo wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Ihefu, kuliwaongezea nguvu ya kupambana na kupata matokeo mazuri michezo miwili iliyopita ikiwa ni njia ya kubeba ubingwa.
Yanga baada ya kupoteza dhidi ya Ihefu kwa mabao 2-1 kabla ya kushinda 3-0 dhidi ya Geita, Simba walishinda michezo miwili iliyofuatia dhidi ya Tanzania Prisons na Singida Fountain Gate.
Akizungumza na Spoti Xtra, Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Simba, Ahmedy Ally, alisema kwa kiasi kikubwa muamko wa ushindi na kupambana ulipatikana baada ya Yanga kupoteza mchezo dhidi ya Ihefu.
“Kusema ukweli baada ya Yanga kupoteza mchezo wao kwa kiasi kikubwa tulipata muamko na hamasa kubwa ya kupambana na kuhakikisha tunashinda michezo yetu yote ili tuweze kukaa kileleni.
“Tunashukuru kwa kweli tumefanikiwa kwa kiasi kikubwa, watu wameona ni kwa jinsi gani timu ilipambana na kweli matokeo yakapatikana, mpaka sasa unaona tunaongoza ligi.
“Nataka niwaambie Wanasimba kuwa malengo yetu msimu huu ni kuona tunafanikisha jambo letu la kutwaa ubingwa baada ya kuukosa ubingwa huu kwa misimu zaidi ya miwili,” alisema kiongozi huyo.
STORI NA MARCO MZUMBE, SPOTI XTRA