Tamasha la Full Dozi Concert litacha historia Dar Live
WAKONGWE wa Muziki wa Kizazi Kipya nchini, Juma Kassim ‘Nature’ na Aboubakar Katwila ‘Q Chillah’ Septemba 9, mwaka huu wanategemea kuliamsha dude katika Ukumbi wa Taifa wa Burudani, Dar Live uliopo Mbagala Zakhem, Dar kwenye shoo ya Full Dozi Concert.
Wasanii hao watashirikiana na wenzao, Snura Mushi, Beka Flavour, Sholo Mwamba, Dully Syskes pamoja na Bendi ya African Stars ‘Twanga Pepeta’ kukamua kwenye tamasha hilo lililoandaliwa na Kituo cha Runinga cha ITV pamoja na Radio One na Capital chini ya kampuni ya IPP Media.
Akizungumza na Risasi Jumamosi, Mratibu wa tamasha hilo, DJ Nico Track amesema kuwa, siku hiyo itakuwa ya makamuzi kutokana na burudani ambayo itaangushwa na wasanii mbalimbali nchini.
“Mara nyingi tumekuwa tukizoeleka kwa upande wa habari za kijamii ambapo sasa tumebadilika na kuja kiburudani zaidi na tumekuja na hili tamasha la Full Dozi Concert ambapo ndani yake kutakuwa na burudani ya kutosha kwa mashabiki na wapenda burudani hapa nchini.
“Listi ya wasanii ambao watapanda jukwaani siku hiyo ya Septemba 9, pale Dar Live wapo wengi na tunaamini kwamba watatoa burudani kwa wote ambao watafika, tena tumeweka kiingilio cha elfu tano tu (5,000) ambacho tunaamini kwamba kila mmoja atakuwa na uwezo wa kukimudu,”alisema mratibu huyo.
Kwa upande wa Meneja wa Dar Live, Juma Mbizo amesema kuwa shoo hiyo itakuwa ya aina yake kutokana na wasanii ambao watalishambulia jukwaa la ukumbi huo.
“Niwaombe wale wote wapenda burudani waje ukumbini siku hiyo, kwani tamasha hili litakuwa la aina yake na linaweza kuvunja rekodi kati ya matamasha ambayo yamewahi kufanyika kwenye ukumbi huu.
“Lakini kila mtu aje akiwa na amani kabisa kwani ulinzi utakuwepo tena wa kutosha na tuna uhakika watakaofika wataliona hilo, siku hiyo milango itakuwa wazi kuanzia saa 2 usiku na hakutakuwa na muda wa kuisha hadi pale utakapoamua kuondoka wewe,”alisema Mbizo.
NA: ALLY KATALAMBULA| GPL