The House of Favourite Newspapers

Tatizo la Mwanamke Kutopata Hedhi

Na Dr. Chale| GAZETI LA IJUMAA | AFYA

Tatizo  la  mwanamke  kutopata  hedhi  yake  kama  kawaida  kitaalamu  inaitwa  Amenorrhea  au inatamkwa  Amenorea. Tatizo  hili  ni  kubwa  na  huwasumbua  wanawake  wengi.

Kufunga  kupata hedhi  kumegawanyika  katika  makundi  matatu;  Kwanza  ni  hali  kitaalamu  iitwayo  ‘Physiologic Amenorrhea’. Hii  inatokea  kabla  msichana  hajavunja  ungo  au  baada  ya  mwanamke  kukoma hedhi, wakati  wa  ujauzito  na  wakati  wa  kunyonyesha, yaani  ni  hali  ya  kawaida,  hapa  siyo  tatizo.

Endapo  mwanamke  alikuwa  anapata  siku  zake  kama  kawaida, halafu  ghafla  zikasimama  asipate tena  kwa  muda  wa  mwezi  au  miezi  kadhaa  na  hana  mimba  basi  hali  hiyo kitaalamu  inaitwa Pathologic,  yaani  kuna  tatizo  linahitaji uchunguzi  wa  kidaktari.

Katika  aina  hizi  mbili  za  kufunga  kupata hedhi   pia  tunaweza  kuzigawa  tena  katika  makundi madogo  mawili  ambayo  ni;  ‘Primary Amenorrhea’,  hapa  msichana  ameshakuwa mkubwa, amepita  umri  wa  kuvunja  ungo   lakini anaweza kuwa  na  tatizo  kubwa  katika  maumbile  yake  ya kike  au  katika  mfumo  wake  wa  homoni  mwilini.

Pia  tuna  hali  nyingine  iitwayo ‘Secondary  Amenorrhea’. Hapa  mwanamke  alishawahi  kupata damu  ya  hedhi  miezi  iliyopita  au  hata  mwaka  lakini  hajaona  tena, wengine  tayari  wana  historia kuwa  walishawahi  kuzaa  lakini  baada  ya hapo  wakafunga  kabisa  kupata  hedhi. Hili  ni  tatizo  la kiugonjwa  linalohitaji  uchunguzi  wa  kina.

Tatizo  lingine  la  kufunga  hedhi  ambalo  ni  la  tatu  katika  kundi  la  matatizo  haya  tunaita ‘Functional  Amenorrhea’. Mwanamke  mwenye  tatizo  hili  ana historia  ya  kuruka  miezi  ya  kupata damu  ya  hedhi.

Atasema  anaweza  kupata  damu  ya  hedhi  baada  ya  miezi  miwili  au  mitatu  hadi sita, yaani  mara  miezi  mingine  apate  au  miezi  mingine  asipate. Mwingine  aidha  hadi  atumie dawa  ndipo  apate  hedhi,  asipotumia  hapati  siku  zake au  mwingine  hata  asipotumia  dawa anaweza  apate  hedhi   au  asipate.

CHANZO CHA TATIZO

Hali  ya  kufunga  kupata  hedhi iitwayo  ‘Pathologic’  kama  tulivyokwishaona  ambayo  pia  ina makundi  madogo mawili ya  ‘Primary’  na  ‘Secondary’  ambapo  aidha  mwanamke  tayari  ashapata  hedhi  baadaye  zikapotea  au  ameshafikisha  umri  mkubwa  lakini  hajawahi  kupata  hedhi, linasababishwa  na  mambo  makubwa  manne  ambapo  mwanamke  huyu  anaweza  kuwa  na  yote  au  mojawapo.

Kwanza  ni  kasoro  katika  viungo  vyake  vya  uzazi  kwa  kutokuwa  na  baadhi  ya viungo  na  hivyo  kutokuendelea  kukua  baada  ya  kufikia  umri stahiki  wa  kuvunja  ungo.

Kasoro  hizi  ni  katika  mfumo  wa  uzazi, vifuko  vya  mayai, uke  au   kuziba njia  ya  uke. Chanzo  cha  pili  ni  tatizo  katika  maumbile  au  mwilini  kwa  ujumla.

Hapa  pia  inaweza  kuwa  kasoro  katika  viungo  husika  vya  uzazi, kimojakimoja  au matatizo katika  mfumo  wa  mwili   inayosababishwa na  unene  au  uzito  mkubwa,  lishe  duni  na kukonda  sana  hasa  kwa  warembo  wanaotaka  wawe  na  umbile  dogo  na  jembamba  na  maradhi mengine  kama  ugonjwa  wa  kisukari.

Vilevile  maambukizi  sugu  husababisha  tatizo  hili  la  hedhi, mfano  ugonjwa  wa  kaswende,  kifua kikuu  na HIV.

Chanzo  cha  tatu  ni  hali  ya  kisaikolojia  ambayo  anaweza  akawa  nayo mwanamke  mwenyewe  au inasababishwa  na  hali  ya  mazingira  anayoishi  au  kukutana  nayo. Matatizo  hayo  ya  kisaikolojia yanaweza  kutokana  na  migogoro  mbalimbali  ya  kiuhusiano, kifamilia  na  kijamii, mishtuko kutokana  na  matatizo  na  kukufanya  akili  isikae  sawa.

Pia kupoteza  hamu  ya  kula kutokana  na  kuogopa  kunenepa  au  kupata  hali  fulani  unayohisi inaweza kutokana na kula chakula, kwa hiyo  unakuwa  na  woga kula chakula au unachagua aina ya vyakula.

Chanzo  cha  nne  ni  matatizo  katika  mfumo  wa  homoni  au  vichocheo  vya  mwili  vinavyoendesha na mfumo  wa  uzazi.

 

UCHUNGUZI NA TIBA

Tatizo  hili  huchunguzwa  na  kutibiwa  katika  kliniki  za  magonjwa  ya  kinamama  kwenye  hospitali za  mikoa. Vipimo  mbalimbali  hufanyika  kutegemea  na  historia  ya  ugonjwa. Vipimo  vya  damu, X-ray,  Ultrasound na  vingine ambavyo  daktari  ataona  vinafaa  utashauriwa.

 

Comments are closed.