TGNP Yawaunganisha Wanavikundi na Wataalamu wa Teknolojia kutoka Chuo cha DIT
MTANDAO wa Jinsi nchini (TGNP) umeingia makubaliano na wataalamu kutoka Chuo cha Teknolojia cha DIT kwa ajili ya kuboresha uwezo wa wanavikundi walioundwa na mtandao huo kwa ajili ya kuboresha kiteknolojia shughuli zao za kiujasiriamali wanazofundishana kwenye vikundi hivyo.
Akizungumza kwenye ufunguzi wa mkutano huo uliofanyika Makao Makuu ya TGNP, Mabibo Dar es Salaam, Afisa TGNP, Florah Ndaba amesema lengo la mkutano huo ni kuwaboreshea uwezo wanavikundi hao walianzishwa na mtandao huo kutokana na changamoto ya kiteknolojia wanazokumbana nazo kwenye uzalishaji wao.
Florah amesema vikundi hivyo vilivyoanzishwa na TGNP vinatoka kata mbalimbali za jiji la Dar, ikiwemo Kata za Saranga, Kivule, Majohe, Manzese, Mabibo na Mabwepande ambapo lengo lake kubwa na kuboresha maisha kupitia ujasiriamali.
Miongoni mwa changamoto waliyoitoa wanavikundi hao kwa wataalamu hao kitendo cha kutengeneza juisi na ikipitisha siku moja inaharibika wakati wafanyabiashara wakubwa wa viwandani juisi zao zinadumu kwenye chupa hata zaidi ya mwaka bila kuharibika.
Kikundi cha Mabwepande ambao wameanzisha mradi wa kutengeneza pilipili na achali nao waliwaeleza wataalamu hao jinsi wanavyopata tabu ya kusindika bidhaa zao na ugumu wanaopitia katika mradi huo.
JINSI YA KUTENGENEZA JUISI KIUJASIRIAMALI NA ISIHARIBIKE MAPEMA
Wanavikundi hao walipotaka kujua jinsi ya kutengeneza vinywaji visivyoharibika mapema walifundishwa jinsi ya kuyahifadhi na kuyasindika matunda ya juisi hiyo na namna ya kufanya kisha kuelekezwa vitu vya kuchanganya ili kulinda ubora wa juisi hiyo ili idumu kama zile za viwandani.
Wanakundi kutoka Mabwepande wao walifundishwa jinsi ya kusindika pilipili zao malighafi wanazotakiwa kuweka kuongezea kwenye bidhaa yao ya achali ili iweze kuwa bora na kudumu muda mrefu bila kuharibika.
SARANGA WAISHUKURU TGNP
Katika mkutano huo wanakikundi kutoka Kata ya Saranga waliishukuru TGNP kwa kuwaanzishia kikundi hicho kilichowapa ubunifu wa kuzigeuza taka kuwa fursa kwa kutengeneza mbolea ambapo kupitia mradi huo kwanza wameondoa tatizo la taka kwenye kata hiyo na pili kujiingizia kipato kwa kuuza mbolea.
Wanakikundi hao wamesema kufuatia mradi huo uongozi wa kata hiyo umewapa tenda ya kuzoa taka ambayo nayo ni fursa nyingine ya kujiingizia kipato kwenye kikundi chao.
Wanakikundi kutoka Majohe nao waliishukuru TGNP kwa kuwaunganisha kwenye vikundi vya ujasiriamali na kuwawezesha kupata ujuzi wa kutengeneza mkaa kwa kutumia makaratasi na kutengeneza mazulia mradi ambao umeanza kuwapatia kipato na kwa maboresho ya kiteknolojia watakayoyapata kutoka kwa wataalamu hao wanatarajia kufika mbali zaidi katika mradi huo. HABARI/PICHA NA RICHARD BUKOS /GPL