The House of Favourite Newspapers

Ukiwa na Mtu wa Hivi, Utainjoi Maisha!

0

JUMAMOSI nyingine Mungu ametupa zawadi ya uhai. Tunaendelea kuomba huruma yake, atuepushe na atuondolee kabisa gonjwa hili la Corona. Tunaamini litaondoka na watu wote watarudi kwenye shughuli zao za kawaida.

Tukirudi kwenye mada ya leo, kama ambavyo inajieleza hapo juu. Kwenye maisha ya uhusiano kila mtu anatamani pengine awe kwenye eneo salama. Aweze kujivunia uwepo wake kwenye mahusiano. Lakini bahati mbaya inawezekana kwa namna moja au nyingine usiweze kumpata mtu wa hivyo.

 

Hii ni kutokana na changamoto ya tabia za watu. Kila mtu ana tabia za aina yake. Alivyolelewa huyu ni tofauti na yule. Ni kama vile nywele. Kila mtu ana zake. Binadamu wote hawawezi kuwa sawa. Kikubwa hasa ni mtu kuamua kujisahihisha kila siku.

 

Kukubali kujifunza tabia njema kila siku. Watu wengi waliofanikiwa duniani, waliamua kubadilika. Watu hawa unaweza kukuta wana historia mbaya ya nyuma lakini mambo yalibadilika kwenye maisha yao pale tu walipoamua kubadili tabia zao.

Mathalan, mtu alikuwa na tabia ya uzinzi, kutumia fedha vibaya au nyingine zinazofanana na hizo lakini akiamua kubadilika na kuwa mtu wa kutunza fedha na kuacha tabia ya uzinzi, mara moja anaanza kuyaona mabadiliko.

 

Mabadiliko haya si kitu cha kulala na kuamka, bali yanafuata mfumo wa muda mrefu. Yanategemea na nidhamu yako katika kusimamia yale mabadiliko unayotaka kuyafanya. Ni rahisi kubadilika leo katika suala fulani lakini usipokuwa makini, kesho unajikuta umerejea kulekule.

 

Lakini unaposimamia mabadiliko yako, utajikuta unaona fedha zako zinakaa benki unaweza sasa hata kufikiria kufanya biashara mpya. Kuijaribu ile biashara na hatimaye kuweza kuifanya kwa nguvu na akili zote. Vivyo hivyo kwenye masuala ya mahusiano, mtu inabidi ubadilike ili uweze kuishi na mtu vizuri.

 

Ukubali akili yako kujifunza tabia mpya na njema kila siku. Kuna mambo ni vigumu kidogo kuyaacha kutokana na mazoea ambayo pengine umejijengea kwa miaka nenda rudi lakini ifike mahali uamue. Weka juhudi kwani hayo ndio maisha yako.

Mtu mzuri kwenye mahusiano ni yupi? Jibu ni rahisi tu, ni yule ambaye anakuwa yupo kwa ajili yako. Ni mtu ambaye yupo kwa ajili ya kukupa faraja. Ni mtu ambaye anakufikiria wewe hata kama haupo. Mtu anayekufikiria wakati haupo maana yake anakupenda.

 

Ni mtu ambaye anakuthamini. Anajitoa kwako katika shida na raha. Kwa hali yoyote, yupo kwa ajili ya kukutia moyo. Mtu ambaye anakuwazia mambo mazuri. Ambaye ni msaada wa wewe kutimiza malengo yako.

Anafahamu jitihada anazozifanya mwenzake, hivyo anamtia moyo, hata kama imetokea ameanguka kwa namna moja au nyingine, atamtia moyo. Atamshauri nini cha kufanya ili aweze kuinuka tena. Anayekupenda anakupigia simu si kwa sababu ana ishu ya msingi, bali anataka tu kusikia sauti yako.

 

Anakupa kipaumbele kwa sababu anakupenda, hakufanyi wa ziada. Huyo ndio mtu unayetakiwa kuwa naye. Ndivyo wewe unavyotakiwa kuwa. Zishike sifa hizo. Zitakusaidia. Kama unajiona una upungufu mahali, jitahidi kubadilika.

Tukutane wiki ijayo kwa mada nyingine nzuri. Unaweza kunifuata kwenye kurasa zangu za mitandao ya kijamii, Instagram&Facebook: Erick Evarist, Twitter: ENangale.

Je, ingekuwa wewe ungefanyaje? Tuma maoni yako kupitia namba 0768 811 595

Leave A Reply