Na Sweetebert Lukonge | CHAMPIONI
MSHAMBULIAJI wa kimataifa, Mtanzania, Thomas Ulimwengu ambaye kwa sasa anacheza soka la kulipwa nchini Sweden, katika Klabu ya AFC Eskilstuna inayoshiriki Ligi Kuu ya nchini humo, hatajiunga na kikosi cha timu ya taifa, Taifa Stars kilichoanza kambi yake jana Jumapili jijini Dar es Salaam.
Stars inajiandaa kwa ajili ya kucheza mechi mbalimbali za kirafiki ili kujiandaa na michezo yake ya kuwania tiketi ya kufuzu kushiriki fainali za Mataifa ya Afrika za 2019.
Akizungumza na Championi Jumatatu, Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Alfred Lucas, alisema Ulimwengu hatajiunga na kambi hiyo kutokana na kuwa majeruhi, hivyo uongozi wa klabu yake ya AFC Eskilistuna umedai kuwa haupo tayari kumuachia.
“Sababu kubwa ya kufanya hivyo ni kile ilichodai kuwa hivi sasa yupo chini ya uangalizi maalumu ili kuhakikisha anapona mapema. “Kutonana na hali hiyo Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Salum Mayanga amesema kuwa hataongeza mchezaji mwingine kwani washambuliaji waliopo katika kikosi hicho kwa sasa wanatosha,” alisema Lucas.
Comments are closed.