The House of Favourite Newspapers

Ruge Afunguka Jinsi RC Makonda Alivyovamia Clouds TV Usiku na Bunduki

Mkurugenzi wa Vipindi na Uendeshaji  wa Kituo cha Clouds Media Group, Ruge Mutahaba amehojiwa leo katika kipindi cha 360 cha televisheni ya Clouds na kuthibitisha kuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda alivamia kituo hicho..
 
Akizungumza na watangazaji wa kipindi hicho, Ruge aliongea kwa hisia na kuthibitisha kuwa tukio hilo lilitokea siku ya ijumaa ya tarehe 17 majira ya usiku kituoni hapo.
 
Alieleza kuwa, siku ya Alhamisi RC makonda alifika katika kituo hicho na kuongea na watangazaji wa SHILAWADU, Sudy Brown na Qwisser ambapo alisema kuwa wanapiga tu stori.
Waziri Nape akiingia kwenye ofisi za Clouds Media na kupokelewa na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni hiyo, Joseph Kusaga.
 
“Mtangazaji mmoja alinifuata akaniambia wamefanya mahojiano na mwanamke anayedaiwa kuwa amezaa na Askofu Gwajima lakini Gwajima mwenyewe hawajampata. Niliwaambia watangazaji kama hawajampata Gwajima, basi kipindi hicho kisirushwe kwa kuwa hakina ‘balance’ na wamwambie Makonda.”
 
Gwajima alinipigia simu akisema amesikia kuwa kuna kipindi chake, nikamwambia kuwa hakitarushwa kwa sababu hatujasikia pande zote. Na nikampigia simu mkuu wa vipindi kumwambia ahakikishe kuwa kipindi hicho hakirushwi kwa vile hakijabalance.”
 
“Ijumaa saa 5 usiku nikapigiwa simu na Afisa Rasilimali Watu wa Clouds kuwa Makonda amekuja ofisini  akiwa na Askari na wana bunduki. Mlinzi hakusita kumruhusu aingie kwa vile amemzoea Makonda, ila alishtushwa na Askari wale waliokuwa na Bunduki.”
 
“Nilimwambia mlizi aende juu studio aone kuna nini na alipokwenda alimkuta Makonda anachukua kipindi kwenye ‘flash’ kisha akaondoka nayo. Hakuna kijana yeyote aliyepigwa usiku ule lakini tatizo kubwa ni namna tukio zima lilivyotokea.”
 
“Makonda alikuja pale na Askari baada ya kuona kipindi chake hakirushwi, hivyo ni kama alikuja kuhoji sababu za kutorushwa kwa kipindi hicho.” Alisema Ruge Mutahaba wakati wa mahojiano leo asubuhi.
RC Makonda
Akizungumza kuhusu video za kamera za ulinzi (CCTV) zilizosambazwa kwenye mitandao ya kijamii, Ruge alikiri kuwa video hizo ni za Clouds lakini hajui ni nani alizitoa kwa sababu wafanyakazi wengi wanafahamu mitambo ya CCTV ilipo hivyo yeyote anaweza kutoa.
 

Vilevile Ruge ameeleza kuwa amesikitishwa sana na kitendo alichokifanya rafiki yake Paul Makonda kwani kilikuwa ni kitendo cha kuivunjia heshima Clouds Media Group pamoja na wadau wengine.

“Makonda tumesaidiana sana tangu akiwa mkuu wa Wilaya. Kwa nini leo anafika kuja ofisini kwangu na bunduki?” alisema.

 
“Makonda ni mkuu wa mkoa wa Dar es salaam lakini ni mdogo sana kwangu kiumri, lazima tuheshimiane. Sijayasema haya kwa sababu nataka mtu atumbuliwe, bali nataka heshima kwenye kile tunachokifanya.”
 
“Sasa tunakuwa tunampa Rais Magufuli mambo mengine ya kufanya ambayo hakutakiwa kuwa anayawaza.”
 

Pamoja na hayo aliongeza kuwa, wao kama Clouds Media Group hawana ugomvi na serikali na ameahidi kutoa nafasi kwa kiongozi yeyote mwenye ajenda ya maendeleo kuja Clouds na atapewa muda wa kuzungumza.

“Sisi tunatafuta viongozi wabunifu. Viongozi wanaokuja na mipango inayoweza kumwezesha mnyonge kuuona mwanga. Viongozi wanapaswa kufanya mijadala ya namna ya kuongeza maendeleo. Inapaswa tushirikiane kutengeneza timu moja na kushirikiana.”

 

Mkurugenzi Ruge Mutahaba, alimaliza kwa kusema kuwa amelizungumzia jambo hilo leo ili limalizike na watu waendelee kufanya mambo mengine ya kuisaidia nchi kimaendeleo.

Vilevile amewataka viongozi na wanasiasa kutokushindana kupata ‘kiki’ kupitia vyombo vya habari na mitandao ya kijamii.

 

Comments are closed.