The House of Favourite Newspapers

Vodacom Yatangaza Kukua Kwa Biashara, Yaendelea Kuongoza katika Umiliki wa Soko la Wateja.

0

Kampuni ya simu za mkononi inayoongoza kidijitali nchini, Vodacom Tanzania PLC imetoa matokeo ya awali ya kifedha kwa mwaka unaoishia tarehe 31 Machi 2020, ikionyesha ukuaji wa kibiashara unaodhihirishwa na ongezeko la umiliki wake wa soko kufikia asilimia 32.8 baada ya kuongeza idadi ya wateja wake kwa kiasi cha milioni 1.4 na kufikisha wateja milioni 15.5.

 

Akielezea kuhusu matokeo ya jumla, Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom Tanzania PLC, Hisham Hendi amehusisha ukuaji wa mapato wa asilimia 0.9 kuwa yametokana na huduma na utekelezaji thabiti wa mikakati ya kibiashara unaowezeshwa na ukuaji thabiti wa idadi ya wateja. Ukuaji mdogo katika nusu ya pili ya mwaka kwa sehemu kubwa ulitokana na matokeo ya kufungia  wateja milioni 2.9 ambao hawajasajiliwa kwa kutumia alama za vidole na gharama zinazohusiana na kukidhi miongozo ya mamlaka pamoja na ushindani mkubwa wa bei.

 

“Wateja wetu wanaendelea kunufaika na mtandao bora wa kiwango cha juu wa Vodacom kutokana na uwekezaji mkubwa wa shilingi bilioni 154.6 katika kuongeza upatikanaji wa mtandao wa 4G na kuboresha ubora wa mtandao na huduma zetu,” alisema Hendi.

 

Kwa kuongezea, alisema kwamba kufuatia kuboreshwa kwa huduma za malipo ya kidijitali; Mapato ya M-Pesa yameripotiwa kuongezeka kwa asilimia 7.4 ambayo imechangia asilimia 35.0 katika mapato ya huduma kufikia 2.2pp inayotokana na kuongezeka kwa idadi ya miamala kwa kila mteja.

 

“Huduma yetu ya M-Pesa imeendelea kutimiza ahadi yake ya kuleta ushirikishwaji wa kifedha nchini Tanzania, kuwawezesha wateja kufanya miamala kwa urahisi na kuchangia katika kukua kwa uchumi. Kwa sasa tuna wateja milioni 10.1 wanaotumia huduma hii ya M-Pesa ambao wamefanya miamala bilioni 1.4 yenye thamani ya shilingi trilioni 58.1 katika mfumo wa huduma za kifedha kupitia simu za mkononi kwa mwaka,” alisema Hendi huku akiongeza kwamba Vodacom itaendelea kupanua mfumo wa M-Pesa kwa kutoa huduma zaidi ili kukidhi mahitaji ya sasa ya wateja kwa kadri yanavyoendelea kubadilika.

 

Taarifa inaonyesha ongezeko la asilimia 9.8 katika mapato yatokanayo na Data ambayo inachangia kiasi cha asilimia 17.7 katika mapato ya huduma, kufikia 1.5pp, mafanikio yanayowezeshwa na mahitaji thabiti ya data, uwekezaji katika mtandao wa data na ongezeko la simujanja nchini.

 

“Tumefanya maendeleo makubwa mwaka uliopita katika kutoa kipaumbele kwenye ushirikishwaji wa kifedha kupitia mfumo wetu wa huduma za kifedha kwa kupitia simu za mkononi, M-Pesa. Wakati huohuo tukiwezesha jamii ya kidijitali kwa kupitia uunganishwaji. Hii inajumuisha kutambulisha simujanja ya bei nafuu shilingi 50,000 (karibu Dola 25), kuongeza huduma zaidi za M-Pesa kama vile bidhaa zetu za malipo ya ziada (Overdraft) pamoja na kuboresha mfumo wetu wa kutuma fedha kimataifa, mambo ambayo yamewezeshwa na uwekezaji endelevu katika mtandao,” alifafanua Hendi.

 

Mkurugenzi aliongeza kwamba, “juhudi hizi zitasaidia kwa kiasi kikubwa ongezeko la wateja wetu na inatarajiwa kuwa kichocheo kikubwa cha ukuaji hapo baadae. Tumeboresha huduma zetu za kidijitali kwa malengo ya kuwapatia wateja wetu huduma zaidi kupitia mifumo ya kidijitali na kutengeneza vyanzo mbalimbali ya mapato.”

 

Akitoa maoni kuhusu matazamio kwa mwaka huu, Hendi alisema, “kufuatia mlipuko wa ugonjwa wa COVID – 19 ambao unaathiri mataifa na wananchi duniani kote, kipaumbele cha Vodacom Tanzania ni katika afya na usalama wa wafanyakazi wetu wakati tukitoa huduma na msaada kwa wateja wetu pamoja na kusaidia serikali pale inapowezekana, kwa ajili ya kukabiliana na hali ya ugonjwa wa COVID – 19.”

 

Aliongeza; “tunaendelea kufuatilia kwa karibu miongozo mipya kutoka Shirika la Afya Duniani pamoja na mamlaka za afya za ndani na kuwa na mpango bora na endelevu wa biashara kwa ajili ya kukabiliana na matukio kama haya. Tuna timu imara inayofanyakazi na kudumisha kiwango cha huduma ambacho wateja wetu wanatarajia kutoka kwetu, lakini pia tumeanzisha huduma mbalimbali za kidijitali ili kuwasaidia wateja wakubwa”.

 

Hendi alimalizia kwa kusema “tunatarajia janga la ugonjwa wa COVID – 19 kuwa na athari katika uendeshaji na utendaji wetu wa kifedha hasa katika nusu ya kwanza ya mwaka. Uongozi unafuatilia hali  inavyoendelea na kushughulikia kwa haraka changamoto zinazojitokeza. Mpaka sasa hatujakumbwa na changamoto inayoweza kukatisha huduma zetu, tunafuatilia kwa makini hali inavyokwenda huku tukiwa tumejiandaa vilivyo kukabiliana na tatizo lolote iwapo litajitokeza,” alihitimisha  Hendi.

 

 

Leave A Reply