The House of Favourite Newspapers

Waheshimiwa Ummy na Ndugulile, Tekelezeni Alichokiagiza Mheshimiwa Rais Juu ya Aga-Khan

0
Rais Magufuli akiteta jambo na Mtukufu Aga- Khan (kushoto).

MOYO wangu uli­jaa hamu kubwa ya kufikisha ujumbe kwa Mtukufu Aga- Khan, tena mbele ya Mhesh­imiwa Rais wa Jamhuri ya Mu­ungano wa Tanzania, kwamba hospitali yake ilikuwa ikiteleza katika utoaji wa huduma, hasa kitendo cha kukataa kupokea wagonjwa waliotumia Bima ya Afya ya Taifa (NHIF).

Wakati ninampa maelekezo Katibu Mhutasi wangu kuan­daa bango ambalo ningeenda nalo Uwanja wa Ndege wa Mwalimu JK Nyerere wakati wa mapokezi ya Aga-Khan, ilikuwa ni mchana wa siku ya Oktoba 10, 2017, siku iliyofuata ndiyo Aga-Khan angewasili nchini saa nne asubuhi!

“Hakikisha bango hilo linakuwa tayari kufikia kesho saa moja asubuhi, umenisikia Glory?”

“Nimekusikia.” Alinijibu kwa njia ya simu kutokea mapokezi.

Ukiwa na siri nzito moy­oni, kuna mambo hutakiwi kumshirikisha mtu yeyote, hata mkeo au mtu mwingine anayekupenda au kukutakia mema, nikalala mpaka asub­uhi ingawa usingizi wangu ulikuwa wa mang’amung’amu, kichwani nikifikiria ambacho kingetokea uwanja wa ndege, pale ambapo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania an­genishuhudia katikati ya watu, peke yangu tu nikiwa nimeshi­ka bango lenye maandishi: “Mr President ask Aga-Khan, why doesn’t he accept NHIF Insur­ance at his main hospital, while he doesn’t pay us tax?”

Kama kawaida ya binada­mu unapowaza, kuna upande utakueleza unachokifanya siyo sahihi, mara nyingi upande huu huonekana kuwa na nguvu za­idi ya ule unaokuambia ni sa­hihi, ndivyo ilivyokuwa, nilianza kusikia sauti zikiniambia: “Rais atakasirika.” Niliamua kuzipu­uza sauti hizo kwa sababu nil­iamini katika kitu nilichokuwa nikikipigania, nikasema: “Litakalokuwa na liwe!”

Niliamini na mpaka sasa ninaamini kitendo cha Hos­pitali ya Aga-Khan, kubwa na yenye vifaa vya kisasa kuliko hospitali nyingi nchini Tanza­nia, haitendi haki kwa Watan­zania inapogoma kupokea na kutibu wagonjwa wenye bima za afya! Hilo ndilo nililokuwa nikilipigania.

Nilijua na ninajua kwamba Hospitali ya Aga-Khan inaweza kujitetea kuwa inapokea wag­onjwa wa bima ya afya kwenye hospitali zake za pembeni, ambazo kwa hakika hazina vifaa wala madaktari bingwa wa kutosha, hawafanyi hivyo kwenye hospitali yao kubwa yenye vifaa vyote na madak­tari wa kutosha, najua pia wa­napokea wagonjwa wa bima ya afya wa daraja la juu kama wabunge n.k.

Nilichokuwa ninakipigania hapa kwanza ni usawa, haki ya kupata matibabu na kuishi ni ya kila Mtanzania na Seri­kali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilianzisha Mfuko wa Bima ya Afya ili wananchi wake waweze kupata matibabu popote, sasa iweje Aga-Khan wakatae kwenye hospitali yao kubwa na kuwasukumia wag­onjwa kwenye vihospitali vyao vya pembeni visivyo na hudu­ma nzuri?

Ziko hospitali nyingi tu bin­afsi hapa nchini, zinazokubali wagonjwa wa huduma ya afya, miongoni mwa hospitali hizo ni TMJ, Regency, Tumaini na Bur­han, kwa nini Aga-Khan waka­tae? Kibaya zaidi wakati wa­nawakataa wagonjwa wa bima ya afya hawatulipi kodi yoyote ile kwa kisingizio kwamba ni shirika la kidini lisilotengeneza faida yoyote.

Lisilotengeneza faida? Huu ni uongo wa karne, ukitaka kuthibitisha hili kipimo kama MRI (Magnetic Resonance Im­aging) katika Hospitali ya Aga- Khan kinatozwa shilingi za Kitanzania 720,000 ukiongeza na dawa ya kufanya picha itoke vizuri, yaani ‘contrast’ utalipa 200,000 zaidi, lakini kipimo hicho hicho kwenye hospi­tali inayotulipa kodi, ya TMJ iliyoko Mikocheni jijini Dar es Salaam ni shilingi 670,000 na kwa Muhimbili ambayo ni hospitali ya serikali ni shilingi 320,000, sasa iweje Aga-Khan wadai hawapati faida wakati Hospitali ya TMJ inayolipa kodi serikalini inatoza kiasi kidogo.

Mheshimiwa Rais, Waziri wa Afya, Naibu, Katibu Mkuu wa Wizara na Watanzania wote, wakati umefika serikali yetu kuzichunguza taasisi za kidini, kwani inaonesha baadhi zina­jificha kwenye neno “Taasisi ya Dini” na kukwepa kodi za mabilioni ambayo yangesaidia maendeleo ya taifa letu, siku­baliani kabisa mtu akiniambia eti hospitali kama Aga-Khan haipati faida, wakati gharama zake ni kubwa kuliko hospitali zinazolipa kodi, kujifungua tu katika Hospitali ya Aga-Khan ni shilingi milioni mbili za Ki­tanzania, halafu wanadai ha­wapati faida na tukubaliane nao, no way!

Nilipoingia ofisini asubuhi ya Oktoba 11, 2017 kichwani mwangu nilikuwa nikifikiria kitu kimoja tu; safari ya uwanja wa ndege, dereva alikuwa tayari na nilikuwa nimeomba waandishi wa habari wa Global TV Online niongozane nao ili warushe tukio hilo live, cha kwanza nili­chokifanya ni kumuuliza Kati­bu Mhutasi wangu kama bango lilikuwa tayari.

“Bado halijaletwa.”

“Lazima unanitania, tangu jana?”

“Wanadai wanamalizia na watalileta muda si mrefu.”

“Sawa.”

Mpaka saa tatu kamili, bango lilikuwa halijaletwa, nikaanza kuishiwa na uvumilivu, lakini ilipohitimu saa tatu na nusu ndiyo nikaletewa bango ofisini, tayari nilishachelewa, nis­ingeweza kuwahi uwanja wa ndege tena, nikampigia simu Mtangazaji wa Channel Ten, Said Makala kumuuliza kili­chokuwa kikiendelea uwanja wa ndege, akanieleza Aga- Khan alishawasili na tayari alikuwa njiani kuelekea mjini, Waziri wa Elimu, mama Ndali­chako na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda ndiyo waliompokea.

Nikafungua mlango wa gari na kulitupa bango ndani yake kisha kupandisha tena ofisini kwangu nikiwa nimevunjika moyo, mtu fulani alikuwa ame­kwamisha kazi niliyotaka kui­fanya, bila shaka huyo alikuwa ni Katibu Mhutasi wangu na kijana aitwaye Sebastian Mkude ambaye ana kampuni ya kuchapisha mabango.

“Lakini Mungu anajua kwa nini jambo hili limetokea, pen­gine ningepewa kipigo mpaka kufa, acha nitafute njia nyingine ya kuwasiliana na rais pamoja na Aga-Khan bila kushikilia bango mkononi!” Niliwaza.

Uamuzi huu ndiyo ulifanya wiki iliyopita nianze kuandika kuwasilisha ujumbe wangu juu ya Hospitali ya Aga-Khan kwa serikali na pia viongozi wa juu wa taasisi, waliosoma wiki iliyopita niliandika: “Hospitali ya Aga-Khan lazima ibadilike, vinginevyo itaendelea kucha­fua sura ya kiongozi wao wa dini!”

Sina tatizo lolote na Mtukufu Aga-Khan, mtu huyu amefanya mambo mengi sana kwa ulim­wengu huu, hasa Afrika, am­eokoa maisha ya watu wengi! Lakini hakuna kizuri kisicho na kasoro, wala sina chuki binafsi na Hospitali ya Aga-Khan, Dar es Salaam, imekwishasaidia familia yangu mno, hasa mama yangu, ninachokifanya hapa ni kutaka hospitali hii ibadilike na kuwa bora.

Mimi kuwa na uwezo wa ku­mudu kulipia matibabu ya Hos­pitali ya Aga-Khan, haitoshi, kuna Watanzania wengi wasio na uwezo huo, lakini wanahi­taji kuishi, hatuwezi kukubali wawekwe pembeni, binadamu wote ni sawa, maisha yangu mimi hayawezi kuwa bora kama ya mwingine hayajawa! Hii ndi­yo sababu ninapiga kelele, niki­taka Hospitali ya Aga-Khan ipo­kee wagonjwa wa bima ya afya, sitanyamaza mpaka jambo hili litokee.

Jioni ya siku aliyowasili Mtukufu Aga-Khan, nikianga­lia taarifa ya habari nyumbani, nilimshuhudia Rais John Pombe Magufuli, rais wa wanyonge, akiongea bila kupindisha kilekile kilichokuwa kichwani mwangu kwamba, Hospitali ya Aga-Khan ilikuwa hailipi kodi na bado gharama zake za matibabu zi­likuwa juu kupindukia, moyo wangu ulijawa na furaha baada ya rais kutamka maneno hayo.

Matumaini yangu ni kwamba kauli ya rais haitachukuliwa kwa wepesi na Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu pamoja na Nai­bu Waziri, Faustine Ndugulile, rais amekwishatamka, wanach­otakiwa kufanya sasa ni kuifua­tilia hospitali hii ili kuhakikisha gharama zake zinakuwa nafuu na wananchi wote wanatibiwa hapo, kutotekeleza jambo hili ni kumpuuza kiongozi wa juu jam­bo ambalo hakika si jema.

Kama rais ameweza kuwa­bana Acacia ambao kwa miaka mingi walipigiwa kelele wak­idaiwa kuliibia taifa letu, in­ashindikanaje kuibana hospitali kama Aga-Khan ili itende haki? Au inaogopwa kwa sababu Mtukufu Aga-Khan alikuwa rafiki wa Mwalimu Nyerere? Au kwa sababu anamiliki vyo­mbo vya habari hivyo anaweza kuipeleka nchi huku au kule ap­endavyo?

Ndugu zangu, kila zama na wafalme wake, utawala uliopo ni lazima uhakikishe kila kitu kinakwenda sawa na kwa Aga- Khan ni kuhakikisha tu matiba­bu yake yanakuwa na gharama za kawaida na pia apokee wag­onjwa wa bima ya afya, nalise­ma hili kwa faida ya Watanzania walio wengi, wasio na uwezo wa kumudu gharama za hospitali kama hiyo.

Tuachane na hofu, tutende haki, tutetee wanyonge kama jinsi rais wetu anavyofanya, wapo wazalendo wengi wa­naoweza kusimama na nchi yao kama ilisimama nao wakati wa dhiki, Waziri Ummy Mwalimu, Naibu wake, Faustine Ndugulile, Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Dk. Mpoki Ulisubisya, hamshindwi kulisimamia jambo hili, msaidi­eni Rais, msipofanya hivyo, kwa Jina la Yesu Kristo Mwana wa Mungu aliye hai, msishangae siku moja mtakaponiona na bango langu kwenye lango kuu la kuingia wizarani kwenu.

Mungu ibariki Tanzania,

Mungu mbariki Rais wetu John Pombe Magufuli,

Mungu tubariki Watanzania wote. Ahsanteni kwa kunisoma.

Itaendelea wiki ijayo.

Usipitwe na Matukio, Install App Yako ya Kijanja na Namba Moja Tanzania ya Global Publishers

Android ===>Google Play

iOS ===>Apple Store

LIVE: Taarifa ya Habari ya TBC 1 Jumapili (Oktoba 22, 2017- Usiku)

Leave A Reply