Wataalam 9 wa Ardhi Waliofariki Ajali Waagwa Morogoro – Video
NAIBU Waziri wa Ardhi, Angelina Mabula, amewaongoza mamia ya wananchi katika zoezi la kuaga miili ya wataalam tisa wa wizara hiyo na mfanyakazi mmoja wa Shirika la Plan International ambao walifariki dunia juzi baada ya gari aina ya Land Cruiser walilokuwa wakisafiria kumshinda dereva na kutumbukia katika mto Kilombero.
Miili hiyo ya watumishi hao imeagwa leo Jumatatu, Februari 25, 2019, katika eneo la Uwanja wa Tangani maarufu kama Uwanja wa Taifa, Ifakara mkoani Morogoro, na kushuhudiwa na wananchi mbalimbali sambamba na viongozi wa serikali, siasa na dini, Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, wakuu wa wilaya za Kilombero, Malinyi na Ulanga.
Mabula amebainisha kuwa serikali imebeba jukumu la kugharamia mahitaji yote yanayohusu mazishi ya watumishi hao ambapo mpaka sasa imeshatumia zaidi ya shilingi milioni 96 katika kuratibu suala hilo.
Akitoa salam za pole kwa ndugu na jamaa wa marehemu hao, Mratibu wa Land Tenure Supporting Program (LTSP), Godfrey Machabe, amesema watumishi hao walikuwa waadilifu na wamelitumikia taifa kwa manufaa makubwa na kwamba walikuwa watu muhimu katika sekta ya ardhi nchini.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Dk. Kebwe Stephene Kebwe, amewaomba wananchi kuwa watulivu na kuvitaka vyombo vya usalama kufuatilia kwa kina na kujua chanzo cha ajali ili haki itendeke.
Comments are closed.