Waziri Ndungulile, Makamba Washiriki Maadhimisho ya Huduma ya Malezi
WAZIRI wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Faustine Ndungulile na Mbunge wa Bumbuli, Januari Makamba na viongozi wengine wamehudhuria maadhimisho ya mwaka mmoja wa huduma ya malezi kwenye makao ya Kituo cha Jerusalem kilichopo Kigamboni, Dar.
Katika maadhimisho hayo mgeni rasmi alikuwa ni Mheshimiwa Ndungulile aliyeambatana na Januari Makamba ambaye ni Baba Mlezi wa Kituo hicho na kuyakagua mazingira ya kituo hicho kinachomilikiwa na familia ya Liginiku Milinga na mkewe, Upendo Ngoda. Wakiwa eneo hilo, Ndungulile na wageni wengine walizunguushwa eneo la kituo hicho na kujionea mazingira wanayoishi watoto hao kuanzia sehemu zao za kucheza, kulala na maeneo mengine.
Baada ya kujionea mazingira hayo Waziri Ndungulile aliwapongeza wamiliki wa kituo hicho, Upendo na mumewe Liginiku kwa jinsi wanavyowalea watoto hao katika mazingira mazuri na kutumia nafasi hiyo kuwaomba wahisani mbalimbali kujitokeza kuongeza nguvu katika malezi ya watoto hao. Januari Makamba ambaye ni Baba Mlezi wa Kituo hicho alimshukuru Waziri Ndungulile kwa kukubali kuwa mgeni rasmi kwenye maadhimisho hayo na kuwahamasisha wahisani wengine kujitokeza kuongeza nguvu kwenye malezi ya watoto.
Makamba ameeleza jinsi alivyoguswa na wazo la waanzilishi wa kituo hicho na malengo yao hali iliyomfanya akubali haraka kwa moyo wake wote kuwa Baba mlezi wa kituo hicho na kuahidi kuzidi kukitumikia.
Akizungumza kwenye maadhimisho hayo mwanzilishi wa kituo hicho, Upendo Ngoda alielezea changamoto mbalimbali anazokutana nazo kwenye malezi ya watoto na kusema anamshukuru Mungu kwa jinsi anavyomuwezesha kuzitatua. Amezitaja baadhi ya changamoto kuwa ni kukosa wauguzi kwenye kituo hicho na hivyo kushindwa kuwapokea watoto wenye uhitaji maalum, udogo wa eneo la kituo pamoja na mambo mengine. Akielezea changamoto ya afya amesema kituo chao licha ya kukosa wauguzi lakini watoto wote wamewakatia bima ya afya.
Upande wa elimu amesema watoto wote waliofikia umri wa kwenda shule wamewapeleka shule binafsi ya St. Joseph iliyopo jirani na kituo hicho na tayari wote wameshalipiwa ada. Upendo amesema kituo hicho kinapokea watoto wa kuanzia umri wa siku moja mpaka miaka 6 na kuwalea mpaka watakapojitegemea.
Upendo amesema lengo la kuanzisha kituo hicho kumlea mtoto wa Tanzania ili aweze kuwajibika na kulijenga taifa lake. HABARI/PICHA NA RICHARD BUKOS /GPL