The House of Favourite Newspapers

ZARI AFUNGUKA DIAMOND KUMPA MAFANIKIO MAKUBWA

KUMPIGA teke chura ni kumwongezea mwendo! Hiyo ndiyo kauli inayoshabihiana na kilichotamkwa na mwanadada wa Kiganda, Zarinah Hassan ‘Zari The Boss Lady’ aliyemwambia mpenzi wake wa zamani Nasibu Abdul ‘Diamond’ kuwa ndiye aliyempa kasi ya mafanikio aliyonayo.  Zari amefunguka hayo hivi karibuni alipoonesha picha ya gari aina ya Ferari yenye rangi nyekundu aliyoipa jina la ‘Queenbae’ ikiwa ni siku chache baada ya kufanya kufuru ya aina yake kwa kudaiwa kununua magari ya kifahari matatu mfululizo hali iliyowafanya mashabiki wake wapigwe na butwaa.

Magari ambayo inaaminika Zari ameyavuta fastafasta ni Rolls-Royce, Maserati na Ferari ambapo aliyaweka kwenye ukurasa wake wa Instagram na wananzengo wakaanza kutoa maoni yao. Kwenye maoni hayo, wapo waliompongeza kwa kumsifia kuwa wanaamini anazo fedha za kufanya kufuru hiyo huku wengine wakimponda kwa kusema magari hayo hayawezi kuwa yake na kumhusisha na mpenzi wake mpya maarufu mitandaoni kwa jina la Kingbae.

Baada ya kuona maoni yanakuwa mengi, Zari alilazimika kuwajibu baadhi ya mashabiki wake kupitia kipengele cha Insta-Story ambapo aliwaeleza kuwa anamshukuru Diamond kwani ndiye aliyempa hasira za kutafuta zaidi mafanikio.“Namshukuru X wangu kwa kunichezea na kunifanya nione mbali kwani nimepata mafanikio,” aliandika kwa kifupi Zari. Licha ya mashabiki kumbana sana Zari kuhusu magari matatu mapya anayoonekana kupiga nayo picha akiwa nyumbani kwake huku wengi wakisema yatakuwa ni ya mpenzi wake.

Siku za hivi karibuni Zari amekuwa akionekana mwenye furaha na kutupia picha mitandaoni zinazomwonesha akiponda raha hadi kuwafanya mashabiki waitamani nyota yake. “Natamani unipe nyota yako hata kwa nusu saa na mimi naota kuwa na baby kama wako,” aliandika mmoja wa wafuasi wake.

Zari akamjibu: “Sio uote, sali na kufunga. Mimi nimefanya hivyo kwa takribani mwaka mzima hadi kumpata.” Zari alimmwaga Diamond Februari 14, mwaka jana (Valentine Day) baada ya kueleza kuwa msanii huyo aliyezaa naye watoto wawili amekuwa na ‘mambo mengi’.

Comments are closed.