Basila Aanika Vigezo Vipya Kushiriki Miss Tanzania – Video
MWANDAAJI na msimamizi wa Shindano la Urembo nchini Miss Tanzania, Basila Mwanukuzi ameanika vigezo vipya kwa washiriki wote wenye ndoto za kuwania shindano hilo kitaifa na hata kimataifa.
Akizungumza katika mahojiano na kipindi cha Mid Morning Fresh kinachoruka kupitia radio namba moja ya mtandaoni nchini Tanzania, +255 Global Radio, Basila amesema moja ya vigezo muhimu kwa sasa ni kila mshiriki kuwa na shughuli anayoifanya na kumuweka karibu na jamii inayomzunguka.
Aidha, Basila kupitia Kampuni yake ya The Look amewataka washiriki wajitokeze kwa wingi na wasiogope kushiriki katika mashindano ya urembo ngazi ya taifa kwa kuhofia muonekano wao kwani vigezo ndivyo vitakavyoamua mshindi katika shindano hilo.
Basila pia amezungumzia suala la zawadi kwa washindi walipita kuwa ni kutokana na kutokuwepo kwa wadhamini wa kutosha na kuomba wadhamini kujitokeza ili kuweza kutumia shindano hilo kama fursa ya kujitangaza.
Mwanukuzi ambaye pia ni mshindi wa mashindano hayo mwaka 1998 amesema licha ya changamoto zilizokuwepo malengo yake ni kuendelea kupeperusha bendera ya Miss Tanzania.