The House of Favourite Newspapers

Cristiano Ronaldo Ataka Kurudi Man United

Cristiano Ronaldo

KOCHA wa zamani wa Real Madrid na England, Fabio Capello amefichua kuwa Cristiano Ronaldo anataka kurudi Manchester United ili aungane na mreno mwenzake Jose Mourinho.

 

Kitendo cha Zinedine Zidane kuachia ngazi kuinoa Real Madrid kimezua hali ya taharuki ndani ya klabu hiyo, ambapo sasa mustakabali wa nyota wawili wa timu hiyo Ronaldo na Gareth Bale umekuwa suala gumu.

 

Nyota hao wawili kwa sasa wanahusishwa na kujiunga na Manchester United kwa ajili ya msimu ujao.

 

Ronaldo alizua mtafaruku baada ya mechi ya fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya Liverpool, ambapo aliwashukuru mashabiki wa Real kwa ushirikiano waliompa kipindi alichokuwa katika timu hiyo akiashiria kama anawaaga.

 

Kwa miaka mwili sasa kumekuwa kuna uvumi kuwa staa huyo anataka kuihama klabu hiyo akilalamikia ushirikiano finyu kutoka kwa uongozi.

 

Capello anasema kutokana na Ronaldo na Mourinho kufanya kazi pamoja Real Madrid kuanzia 2010 na 2013 walijenga uelewano mkubwa ukizingatia wote wanatoka Ureno.

 

“Cristiano anataka kurudi Manchester United ili akafanye kazi na Mourinho,” alisema Capello katika mahojiano na televisheni ya Sky Sport 24.

“Ninadhani hatimaye ataondoka Real Madrid na kurudi zake Manchester United alipotengeneza jina lake,” aliongeza Capello.

 

Hata hivyo, uamuzi juu ya mustakabali wa Bale na Ronaldo utawekwa bayana baada ya Real Madrid kupata kocha mpya.

 

Nyota hao wawili walianza kutamba kwenye Ligi Kuu England, ambapo Ronaldo alichezea Manchester United mwaka 2003 hadi 2009 wakati Bale alikuwa Tottenham tangu 2007-2013.

 

Real Madrid inaendelea na mchakato wa kupata kocha mpya huku kocha wa Tottenham Hotspur, Mauricio Pochettino akipewa nafasi kubwa ya kukabidhiwa mikoba ya Zidane.

Comments are closed.