HATIMAYE ile tuzo ya Radio Namba Moja ya Mtandaoni Tanzania iliyotolewa na Tanzania Digital Awards iliyobebwa ‘kibabe’ na +255 Global Radio, imefika salama makao makuu ya Global Publishers Sinza-Mori, jijini Dar es Salaam.
Tuzo hiyo ambayo inatambulika pia kama TDA ililetwa jana Jumatatu na kupokelewa kwa shangwe na watangazaji na waandishi wa Global Publishers Ltd wakiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Global Publishers, Eric Shigongo, Mhariri Mtendaji Saleh Ally (Jembe) na Meneja wa Global Radio, Lucas Masungwa.
Akipokea tuzo hiyo kutoka kwa wawakilishi wa TDA, Jembe alisema: “Hakika imekuwa alama ya kuonyesha kuwa tunafanya kazi nzuri na hapo tulipofika tunatakiwa kwenda mbali zaidi ili mwaka huu tuchukue tuzo nyingine.”
Naye Lucas Masungwa ambaye pia ni mtangazaji wa kipindi cha Front Page aliwataka watangazaji na waandishi wote wa Global kuendelea kushirikiana zaidi kwa sababu tuzo hiyo imepatikana kutokana na ushirikiano wa wafanyakazi wote.
Wakati huohuo, Mkurugenzi Mtendaji wa Makampuni ya Global Group, Eric Shigongo, alitoa wito kwa wafanyakazi kujituma zaidi wakati wakishangilia kupata tuzo hiyo ya ushindi.
Desemba 26, 2020, +255 Global Radio ilitangazwa kuwa mshindi wa Online Radio of the Year ikiziacha kwa mbali radio nyingi nyingine nchini.
Na Issa Liponda